ANGALIA LIVE NEWS

Saturday, March 26, 2016

Kificho ang’olewa uspika

Aliyekuwa Spika wa Baraza la Wawakilishi la Zanzibar, Pandu Ameir Kificho ameangushwa katika kinyang’anyiro cha kuwania tena nafasi hiyo ndani ya CCM.
Kificho aliyeshikilia nafasi hiyo tangu kuanza kwa mfumo wa vyama vingi vya siasa nchini mwaka 1992, ameshindwa nafasi hiyo katika uchaguzi uliofanyika jana katika Ofisi za CCM Kisiwandui mjini hapa.
Mwenyekiti wa uchaguzi huo alikuwa mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM, Balozi Seif Ali Iddi na kuhudhuriwa na wajumbe 72.
Katika uchaguzi huo Zuber Ali Maulid aliibuka mshindi baada ya kupata kura 55 na kumwangusha Kificho aliyepata kura 11 huku Jaji Janeth Nora Sekihola akiambulia kura nne. Kura mbili ziliharibika.
Akizungumzia uchaguzi huo jana, Naibu Katibu Mkuu wa CCM, Zanzibar, Vuai Ali Vuai alisema: “Tumeshamaliza uchaguzi kwa mujibu wa utaratibu wa chama chetu, mshindi wa nafasi hiyo ameshapatikana na jina la mgombea tunalo mkononi sasa.”
Vuai alisema mchakato wa kumpata Spika ulianza baada ya kujaza fomu za maombi, kati ya Machi 22 na 23 na wana-CCM tisa wenye sifa waliojitokeza kuwania nafasi hiyo.
Alibainisha kuwa baada ya hatua hiyo, majina yalijadiliwa katika kikao maalumu cha CCM na hatimaye Kamati Kuu, iliyochuja na kupitisha majina matatu ya wagombea waliochuana kwa kupigiwa kura.
Zuber ambaye sasa anasubiri kupigiwa kura na kuthibitishwa na Baraza la Wawakilishi Zanzibar linalotarajiwa kuketi hivi karibuni katika ukumbi wa Chukwani mjini hapa, aliwahi kuwa Waziri wa Biashara na Viwanda wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ), katika Awamu Sita iliyoongozwa na Amani Abeid Karume.
Pia, kwa vipindi viwili mfululizo, kuanzia mwaka 2000 aliwahi kuwa Mbunge wa Mwembemakumbi Unguja, kabla halijabadilishwa na kuitwa Chumbuni ambako akiwa bungeni aliwahi kuchaguliwa kuwa Mwenyekiti wa Bunge la Tisa lililokuwa likiongozwa na Samuel Sitta.
Zuber ana Stashahada ya ualimu aliyoipata katika Taasisi ya Kiswahili na Lugha za Kigeni Zanzibar (Takiluki), mwishoni mwa miaka ya 1980 na mwanzoni mwa 1990. Pia aliwahi kusoma masomo ya uchumi nje ya nchi.

No comments: