Advertisements

Friday, May 6, 2016

WABUNGE WA UKAWA WAMZOMEA PROFESA TIBAIJUKA HUKU WAKIMWITA MWIZI BUNGENI

Mbunge wa Muleba Kusini (CCM), Profesa Anna Tibaijuka jana alikuwa mkali bungeni akisema yeye si mwizi na kuwabeza wanaomuita hivyo kuwa wataisoma namba.

Profesa Tibaijuka alifikia hatua hiyo baada ya kuhamaki kutokana na baadhi ya wabunge wa upinzani kupaza sauti na kumuita mwizi wakati akichangia hotuba ya bajeti ya Wizara ya Katiba na Sheria.

Profesa Tibaijuka alianza kwa kuwataka wabunge wamuunge mkono Rais John Magufuli kwa kuwa amechaguliwa na wananchi.

“Wenzetu ambao kazi yao ni kuja kutusimamia sisi (upinzani) wana haki ya kusema wanayoyasema, lakini hata sisi tuna haki ya kuyaweka vizuri ili yaeleweke kwa wananchi,” alisema.
Profesa Tibaijuka alisema upinzani ukifilisika utabaki kukemea kwa sababu ni lazima tu useme kitu, Bunge linageuka kijiwe na bungeni si mahali pa kupeleka hoja za vijiweni.

Kauli hiyo iliwakera wabunge wa upinzani ambao walianza kupaza sauti zao dhidi yake, hali iliyoonekana kumchanganya.

Akirejea hotuba ya msemaji wa kambi ya upinzani bungeni, Tundu Lissu kuwa Tanganyika inainyonya Zanzibar na kuifanya koloni lake, Profesa Tibaijuka alihoji: “Tanganyika inainyonya Zanzibar katika lipi? Hili ni jambo la kujiuliza. Nimejiuliza mimi kama mchumi. Kazi yangu ya kwanza nyinyi mnanijua nilikuwa kwenye shirika la makazi duniani, hamjui kwamba nilikuwa kwenye Shirika la Biashara la Dunia?” alihoji.

Kutokana na zomeazomea kuendelea, Spika wa Bunge, Job Ndugai aliingilia kati: “Waheshimiwa wabunge namlinda mzungumzaji, naomba muwe wavumilivu. Mheshimiwa Profesa endelea."

“Kwa wale wanaosema nimeiba mtaisoma namba, mimi si mtu wa kutishwa na vitu vya ovyoovyo.

"Mimi sitishwi na hoja za ovyoovyo, huyo (mtu) akaisome namba. Nasimama hapa kwa sababu nataka nitetee vitu. Mtu anapopotosha anaweza kuleta hatari. Tanganyika kwa mtizamo wa kiuchumi haiwezi kuinyonya Zanzibar.

“Katika Dunia ya ustaarabu unasikia hoja. Lissu hapa angeweza kuzomewa, lakini wastaarabu wakamsikiliza wamekomaa kisiasa,” alisema huku baadhi ya wabunge wakiendelea kumzomea.

Tibaijuka aliwahi kuwa waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi wakati wa utawala wa Rais Jakaya Kikwete na aliondolewa baada ya kutuhumiwa kupata mgawo wa fedha za Tegeta Escrow.

7 comments:

Anonymous said...

Tundu Lisu ni mtu wa kuropokwa hovyo kama kasuku asiejua anachokizungumza ni miongini mwa watu ambao wanaombea utabaka kuota mizizi Tanzania yaani utanganyika,uzanzibari,usukuma,upemba,ubara,uvisiwani ilimradi wanasiasa wa aina ya akina Tundu Lisu ni kuleta fitna Tanzania si vingine labda kwa akili zao za uroho wa madaraka wanaona sera za divide and rule zina weza kufanya kazi kwa wapizani lakini tujiulize ni tangu lini fitna zikazaa kitu kilicho na manufaa katika jamii?

Anonymous said...

Mtoa hoja May 6, 2016 at 8:18am inaonyesha jinsi gani gani akili yako zimegubikwa na fikra za mipasho ma mahaba na CCM. Uchaguzi ZNZ wa kwanza na marudio haukuwa wa haki. Hili halina mjadala.....ni vizuri wewe na wabunge wetu wa CCM kuelewa kwanza wanawakilisha wapiga kura wa jimbo lake, pili wanawakilisha watanzania kiujumla, tatu kufuata yake mwenyewe yenye uzalendo na nchi yake, na labda mwisho kufuata maamuzi ya matakwa ya chama chake....Kwa ujinga huu unaouleta hapa ndio mwendekezo wa fikra za mwenyekiti zidumu....hoja yako ipeleke katika mitandao yenu ya kijinga kuliko humu...

Anonymous said...

Mtoa mada hapa juu. Naona kama ulikuwa unala moyoni kuhusu Tundu Lissu, kwani hapa umetoka nje ya mada kabisa linaloongelewa hapa ni mbunge wa Muleba Kusini A. Tibaijuka unatoka nje ya mada unaenda kumuweka mtu ambaye siye mtajwa na hana jinsi yoyote anaingia kwenye hii mada.
Tatizo letu ni ubaya wa aina ambayo haiwezi kutupeleka tunakotaka lazima tujaribu kuwa na mwelekeo. ungelizungumzia labda wanataka kutaja ya ESCROW wallau ingelingana kidogo. asante.

Anonymous said...

kama ingeleikuwa Lissu yuko katika hiyo position uliomuweka, naamini serikali na kwa vile haiendezwi na anachokisema, sasa hivi angelikuwa ameshachukuliwa hatua. anachokieleza Lissu ni uhalisia uliopo ndani ya tanzania, usilifumbie macho hili kwa vile liko zanzibar, hii sumu itatambaa itakuja hadi mlangoni kwako, ikifikia hapo ndio utajua au kumfahamu Lissu anachokisema.

Anonymous said...

Whoever thinks Tundu Lissu is credible ought to have their heads examined.

Anonymous said...

Liwe swala la zanzibar au wizi wa mama Tibaijuka.hakuna sababu ya wabunge kumzomea na kumvunjia heshima huyu mama.wengine nikama mama yao. Swala la Tibaijuka wangemuuliza Mwakyembe kwanini yule mama yupo bungeni. Wananchi wa muleba walimchagua dhidi ya wapinzani hivyo mpeni heshima yake kama mbunge. Pelekeni malalamiko yenu kwenye jimbo lake na si bungeni kwani vyombo vya sheria vipo. Yawezekana ndiyo maana selikari imefungia matangazo(maonyesho)ya TV,kwakuepuka mambo kama haya. Asanteni.

Anonymous said...

Hela ya mboga....

Kudadadeki!!!