Advertisements

Wednesday, July 27, 2016

CAG ASSAD AONGOZA KIKAO CHA 70 CHA BODI YA UKAGUZI YA UMOJA WA MATAIFA


Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki Moon, akiwa na Wajumbe wa Bodi ya Ukaguzi ya Umoja wa Mataifa, wakati wa hafla fupi ya kumuaga Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali ya Uingereza Sir Amyas Morse ambaye amemaliza muda wake wa uhudumu wa miaka sita katika Bodi hiyo. Hafla hiyo ilihusisha pia kukaribishwa kwa Bw. Kay Scheller Rais wa Ofisi Kuu ya Ukaguzi ya Ujerumani anayechukua nafasi ya Uingereza. Mabadilishano hayo yalikuwa ni sehemu ya Kikao cha 70 cha Bodi ya Ukaguzi ya Umoja wa Mataifa ambayo ipo chini ya Uenyekiti wa Prof Mussa Assad, Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali kutoka Tanzania. Kutoka kushoto ni: Bw. Kay Scheller ( Ujerumani), Sir Amyas Morse ( Uingereza), Katibu Mkuu Ban Ki Moon ( UN), Prof Mussa J. Assad( Tanzania) na Bw. Shashi Kant Sharma ( India)

Mwenyekiti wa Bodi ya Ukazuzi ya Umoja wa Mataifa, Prof. Mussa Assad akizungumza wakati wa hafla ya kuiaga Ofisi ya Mkaguzi na Mdhibiti wa Hesabu za Serikali ya Uingereza ambaye amemaliza ujumbe wake wa miaka sita katika Bodi. Mwenyekiti alitumia fursa hiyo kumshukuru Sir Amyas Morse kwa ushirikiano na weledi mkubwa katika utekelezaji wa majukumu ya Bodi.


Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali, Prof. Mussa Assad akiongoza kikao cha 70 cha Bodi ya Ukaguzi ya Mashirika na Mifuko iliyochini ya Umoja wa Mataifa pamoja na shughuli nyingine zinazohusiana na Umoja wa Mataifa, Kikao hicho cha 70 kilifanyika siku ya Jumanne hapa Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa.

Wajumbe wa Bodi ya Ukaguzi kutoka kushoto , Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa n Hesabu za Serikali ya India, Bw. Shashi Kant Sharma, Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali ya Uingereza, Sir Amyas Morse, na Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali ya Tanzania, Prof. Mussa Juma Assad, wakitia saini zao katika ripoti 11 za ukaguzi wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa zilizorejewa na kupitishwa na Bodi hiyo wakati wa mkutano wake wa sabini (70), uliofanyika siku ya  jumanne hapa Makao Makuu ya Umoja huo, New York, Marekani. Ripoti hizo ni matokeo ya kazi kubwa ya Bodi hiyo.
Ujumbe wa Ofisi ya Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali ( CAG) muda mfupi kabla ya kuanza rasmi kwa kikao cha 70 cha Bodi ya Ukaguzi ya Umoja wa Mataifa. Kutoka kushoto Bw. Isaya Jeremiah, Naibu Mkurugeni Ukaguzi wa Nje, Bw. Jerome Francis, Naibu Mkurugenzi Ukaguzi wa Nje, Bw. Salhina Mkumba, Mkurugenzi wa Ukaguzi wa Nje, na wa mwisho ni Bw. Athuman S. Mbuttuka, Naibu Mkaguzi Mkuu anayesimamia ukaguzi wa Hazina na Umoja wa Mataifa.

Na Mwandishi Maalum, New York
Bodi ya  Ukaguzi ya Umoja wa Mataifa,   ambayo   Mwenyekiti wake ni   Mkaguzi na Mdhibiti  n  Mkuu  wa  Hesabu za Serikali, ( CAG) Profesa Mussa J. Assad jana  ( Jumanne)  imerejea  na kuidhinisha  ripoti  kumi na moja za  Mashirika, Mifuko  na shughuli  mbalimbali za Umoja wa Mataifa.
Katika kikao hicho cha   70 kilichofanyika  hapa  Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa,  pamoja na kuidhinisha ripoti za  Mashirika  na  Mifuko  iliyochini  chini ya Umoja wa Mataifa,  pia Bodi ilipokea  taarifa mbalimbali za kiutendaji zinazohusiana na   majukumu ya  Bodi hiyo.
Wajumbe wa Bodi ya Ukaguzi ya Umoja wa Mataifa, ni    Mkaguzi na  Mdhibiti  Mkuu wa Hesabu wa Serikali ya India,  Bw. Shashi Kant Sharma,    Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali ya Uingereza, Sir Amyas Morse, na Mkaguzi na  Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Prof. Mussa J. Assad.
Pamoja na  kupitia na kuridhia ripoti hizo kumi na Moja, na  kupokea  taarifa za kiutendaji, shughuli nyingine iliyofanywa na  Bodi ya  Ukaguzi ilikuwa ni pamoja na  kuiaga Ofisi ya Ukaguzi ya Uingereza  baada ya  kumaliza  kipindi chake cha miaka sita ya uhudumu katika Bodi hiyo.
Hafla ya  kuagwa kwa   Ofisi  ya Ukaguzi ya Uingereza ilihudhuriwa  na Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa,  Bw. Ban Ki Moon pamoja na wadau mbalimbali ambao ni wateja wa Bodi ya Ukaguzi ya Umoja wa Mataifa.
Nafasi ya  Ofisi ya Ukaguzi ya Uingereza  imechukuliwa na Ofisi  ya Ukaguzi ya Ujerumani ambayo  imekaribishwa  rasmi kuwa mjumbe wa Bodi  hiyo.
Akizungumza katika hafla  hiyo ya kuiaga  ofisi ya Ukaguzi ya  Uingereza na  kuikaribisha Ofisi ya Ukaguzi  ya Ujerumani,  Mwenyekiti wa Bodi,  Prof.  Mussa Assad amemshukuru Sir. Amyas Morse  kwa mchango wake yeye binafsi na Ofisi yake kwa uwajibikaji mkubwa na weledi wa hali  ya  juu ambao umefanikisha utekelezaji  wa mamlaka na  majukumu ambayo Bodi hiyo imekabidhiwa na Umoja wa Mataifa.
Akiikaribisha   Ofisi ya   Mkaguzi  na Mdhibiti Mkuu wa Ujerumani,  Prof. Assad  ameelezea matumaini yake  ya kufanya kazi kwa karibu na ushirikiano wa hali  ya juu na  mjumbe huyo ili  kwa pamoja waweze kutekeleza majukumu na mamlaka  waliyokabidhiwa na  Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa.
Bodi ya Ukaguzi  ya Umoja wa Mataifa, ilianzishwa   mwaka 1946  na Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa kwa lengo la kukagua hesabu za Mashirika,  Mifuko na Taasisi nyingine zilizo chini ya Umoja wa Mataifa,   ili  pamoja na mambo mengine kuhakikisha kwamba Taasisi hizo zinatekeleza majukumu yake kwa mujibu wa kanuni na taratibu za  Umoja wa Mataifa ikiwa ni pamoja na matumizi yenye tija na adilifu ya   bajeti  kulingana na  mamlaka ya   Mashirika na Taasisi hizo.
Bodi ya Ukaguzi inatekeleza majukumu yake  kama chombo huru na taarifa zote za ukaguzi huwasilishwa kwa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa pamoja na wateja  ambao  wanakaguliwa  na  Bodi hiyo.

No comments: