Advertisements

Thursday, July 14, 2016

JK: UTAFITI WA KINA WAHITAJIKA KUKUMBANA NA MABADILIKO YA TABIA NCHI AFRIKA

Rais mstaafu Dkt. Jakaya Kikwete akifungua mkutano wa tatu wa Sera za Mabadiliko ya Tabia Nchi jijini Dar es Salaam iliyoandaliwa na Taasisi ya Uongozi kwa kushirikiana na Climate Strategies. Mkutano huo ilijumuisha watafiti na watunga sera 80 kutoka nchi zaidi ya 10 nje na ndani ya Afrika chini ya kauli mbiu "Kutekeleza Makubaliano ya Paris - Suluhu Mpya za Utafiti kwa ajili ya Nchi zinazoendelea." Kutoka kulia ni Mwenyekiti wa mkutano huo Bw. Chuks Okereke, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais - Mazingira na Muungano Mhe. January Makamba na Afisa Mtendaji Mkuu wa Taasisi ya Uongozi Profesa Joseph Semboja.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais - Mazingira na Muungano Mhe. January Makamba akizungumza katika mkutano wa tatu wa Sera za Mabadiliko ya Tabia nchi unaoendelea jijini Dar es Salaam. Waziri Makamba amesema kwamba Tanzania ni miongoni mwa nchi 175 zilikubali na kutia saini Makubaliano ya Paris Aprili 22 mwaka katika makao makuu ya Umoja wa Mataifa, New York ili kuweza kupunguza na kudhibiti utoaji wa gesi ya kaboni duniani.

Mwenyekiti wa Mkutano wa Sera za Mabadiliko ya Tabia Nchi Bw. Chuks Okereke kutoka Chuo Kikuu cha Reading, Uingereza akizungumza wakati wa ufunguzi wa mkutano huo. Mkutano huu ni wa tatu kufanyika duniani na wa kwanza kufanyika barani Afrika baada ya London, Uingereza 2014 na New Delhi, India 2015.
Washiriki wa mkutano wakiendelea kusikiliza mada mbali mbali kutoka wataalam wa mabadiliko ya tabia nchi. Mkutano huu umewaleta watafiti, watunga sera, na wadau wa mazingita kutoka sekta ya umma, binfasi na taasisi zisizo za kiserikali kutoka nchi 10 ndani na nje ya Afrika kuweza kujadili suluhu mpya za utafiti kwenye mabadiliko ya tabia nchi kwa ajili ya nchi zinazoendelea.
Rais mstaafu Dkt. Jakaya Kikwete katika picha ya pamoja na baadhi ya washiriki wa mkutano wa tatu wa Sera za Mabadiliko ya Tabia Nchi iliyoandaliwa na Taasisi ya Uongozi kwa kushirikiana na Climate Strategies. Dkt. Kikwete alifungua mkutano huo wa siku mbili jijini Dar es Salaam iliyojumuisha watafiti na watunga sera 80 kutoka nchi zaidi ya 10 nje na ndani ya Afrika chini ya kauli mbiu "Kutekeleza Makubaliano ya Paris - Suluhu Mpya za Utafiti kwaw ajili ya Nchi zinazoendelea." Kutoka kulia ni Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais - Mazingira na Muungano Mhe. January Makamba, Mwenyekiti wa mkutano huo Bw. Chuks Okereke, na Afisa Mtendaji Mkuu wa Taasisi ya Uongozi Profesa Joseph Semboja.

Rais mstaafu Dkt. Jakaya Kikwete ametoa wito kwa viongozi serikalini, watafiti, watunga sera, wafanyabiashara, taasisi zisizo za kiserikali na wadau wote wa mazingira kuwekeza katika utafiti utakaotoa majibu na sera sahihi kwa ajili  ya kukumbana na changamoto ya mabadiliko ya tabia nchi barani Afrika.

Rais mstaafu Kikwete alisema hayo wakati anafungua mkutano wa tatu wa Mabadiliko ya Tabia Nchi Duniani inayoeendelea jijini Dar es Salaam, iliyoandaliwa na Taasisi ya Uongozi kwa kushirikiana na taasisi ya kimataifa ya tabia nchi, Climate Strategies.

Mkutano huo unalenga kukuza mjadala kwa ajili ya kutoa muongozo bora ya namna ya kutekeleza maazimio ya Makubaliano ya Paris ya Desemba 2015 katika suala la mabadiliko ya tabia nchi. Kauli mbiu ya mkutano huo wa siku mbili ni “Kutekeleza Makubaliano ya Paris – Suluhu Mpya za Utafiti kwa ajili ya Nchi zinazoendelea.”

“Mabadiliko ya tabia nchi ni hali ya ukweli unaoendelea kuikumba dunia. Kwahiyo kuidhibiti mabadiliko ya tabia nchi kunahitaji namna mpya ya kufikiri na ushirikiano mipya baina ya sekta, mataifa, makazi na jamii mbalimbali duniani,” alisema Rais mstaafu Kikwete.

“Ni kwa sababu hii utafiti una umuhimu mkubwa sana katika kujenga sera ambazo zinazo shabiana na hali halisi kwa ajili ya kukabili na kukubali namna bora ya kupokea matokeo ya mabadiliko ya tabia nchi. Utafiti unapaswa kutoa taarifa sahihi ya nini kifanyike, namna gani ya kufanya, na kwa nini inahitajika kufanyika. Ni kwa njia hii tu sera zetu zitakuwa katika misingi bora zaidi,” alisema.

Aliendelea, “Utafiti utakaofanyika lazima uwe wa kimatendo zaidi na si kinadharia. Pia unatakiwa uwe katika muktadha wa tunu zetu na mazingira ya kwetu Afrika, bila kuitenga dunia.”

Nchi zinazoendelea kama Afrika zinahitaji mfano wake wenyewe wa maendeleo utakaotutoa katika umaskini na kuwapelekea maendeleo jamii zetu. Lazima tutengeneze njia zetu wenyewe zitakazozaa maendeleo endelevu utakao jibu matakwa ya mazingira yetu wenyewe alishauri Rais mstaafu Kikwete.

Wakati huo huo, Waziri wa Nchi wa Mazingira na Muungano Mhe. January Makamba alisema kwa serikali ipo katika mchakato wa kutekeleza Makubaliano ya Paris, ambapo Tanzania ilikuwa kati ya nchi moja wapo 175 duniani zilizokubali kutia sahihi makubaliano hayo katika makao makuu ya Umoja wa Mataifa, Aprili 22 mwaka huu.

“Tupo njiani kutekeleza makubaliano haya nchini. Katika ngazi ya kitaifa, hivi karibuni tumeanzisha Taasisi ya Ufuatiliaji na Udhibiti wa Utoaji wa gesi ya Kaboni katika Chuo cha Kilimo Sokoine, taasisi ya kwanza na ya pekee ya aina yake Afrika Mashariki,” alisema Waziri Makamba.

“Taasisi hii itasaidia kuhesabu na kuelewa utoaji wa gesi  ya kaboni katika hewa yetu na namna gani inavyoathiri misitu yetu na njia mbadala za kuidhibiti na kuizuia  gesi hii ili kuweza kwenda sambamba na Makubaliano ya Paris ambayo inahitaji wadau wake kupunguza utoaji wa gesi hii kwa kiwango fulani,” alieleza.

Mkutano huo wa siku mbili ni mkutano wa tatu kufanyika duniani lakini wa kwanza kufanyika barani Afrika baada ya London, Uingereza 2014, New Delhi, India 2015. Mkutano huu umewaleta watafiti, watunga sera, na wadau wa mazingira kutoka serikalini, sekta binafsi na taasisi zisizo za kiserikali kutoka nchi 10 ndani na nje Afrika.

No comments: