Advertisements

Thursday, August 11, 2016

CHAMA CHA SIASA CHAFUTIWA USAJILI

Msajili wa Vyama vya Siasa  nchini amekifuta katika orodha ya vyama vya siasa vyenye usajili wa muda Chama cha Maadili na Uwajibikaji (CM-Tanzania) kutokana na kushindwa kutimiza masharti ya usajili. Chama cha CM-Tanzania kilipata usajili wa muda tarehe 4 Februari, 2016.

Kwa mujibu wa kifungu cha 8(3) na (4) cha Sheria ya Vyama vya Siasa namba 5 ya mwaka 1992, chama cha siasa chenye usajili wa muda ni lazima kiwasilishe maombi ya usajili wa kudumu ndani ya siku mia moja na themanini tangu tarehe ya kupata usajili wa muda. Aidha, uhai wa chama cha siasa chenye usajili wa muda unaisha baada ya siku mia moja na themanini (180) tangu kipate usajili wa muda .

Hivyo, uhai wa cheti cha usajili wa muda wa Chama cha Maadili na Uwajibikaji (CM-Tanzania) ulikwisha tarehe 2 Agosti, 2016, kwani waanzilishi wake walipaswa kuwasilisha maombi ya usajili wa kudumu siyo zaidi ya tarehe 02 Agosti, 2016.


Kwa mujibu wa Sheria ya Vyama vya Siasa, waanzilishi na wanachama wote wa CM-Tanzania hawapaswi kufanya siasa au shughuli yoyote kwa jina la Chama cha Maadili na uwajibikaji, kwa sababu uhai wa cheti chake cha usajili wa muda umekwisha. Kufanya hivyo ni kukiuka Sheria za nchi.

Kufutwa kwa Chama cha Maadili na Uwajibikaji  kunaifanya idadi ya  vyama vya siasa vyenye usajili wa muda  kuwa kimoja ambacho  ni  Chama cha Restoration of the Nation Party (RNP). Aidha, idadi ya vyama vya siasa vyenye usajili wa kudumu ni ishirini na mbili (22).

No comments: