Advertisements

Thursday, August 25, 2016

NYOSSO KAOMBA KUPUNGUZIWA ADHABU NA TFF


Beki wa zamani wa Mbeya City, Juma Nyosso. 
By Mwanahiba Richard 

KWA UFUPI;-

Nyosso alipata adhabau hiyo mwaka jana baada ya kudaiwa kumfanyia kitendo cha udhalilishaji straika wa Azam, John Bocco na kutakiwa kulipa Sh 2 milioni adhabu ambayo amekuwa akiilalamikia kuwa ni kubwa na inamuumiza kwani tayari maisha yake yameharibika.
BEKI wa zamani wa Mbeya City, Juma Nyosso amewasilisha barua yake rasmi juzi Jumatatu ya kuomba radhi ili apunguziwe adhabu ya kufungiwa miaka miwili kucheza soka katika Ofisi za Shirikisho la Soka nchini (TFF).
Nyosso alipata adhabau hiyo mwaka jana baada ya kudaiwa kumfanyia kitendo cha udhalilishaji straika wa Azam, John Bocco na kutakiwa kulipa Sh 2 milioni adhabu ambayo amekuwa akiilalamikia kuwa ni kubwa na inamuumiza kwani tayari maisha yake yameharibika.

Hivi karibuni, Nyosso alilieleza Mwanaspoti kuwa anashindwa kumudu kuendesha familia yake kwani hana kazi yoyote na amekuwa akisaidiwa na marafiki na hivyo kuiomba TFF impunguzie adhabu hiyo na ikiwezekana naye aitwe kujieleza.

Meneja wa mchezaji huyo, Herry Mzozo alisema kuwa kwasasa wanasubiri uamuzi wa TFF kwani tayari wamepeleka barua hiyo juzi Jumatatu ili wasikiliwe ombi lao na kama ikiwezekana afutiwe adhabu hiyo.

“Nyosso hana ajira nyingine zaidi ya soka, maisha yake yamekuwa magumu na ana familia, tumeandika barua ya kuomba radhi na tumeipeleka TFF ambapo tunaamini Katibu Mkuu anajuwa sehemu sahihi ya kuipeleka ili ifanyiwe kazi, Nyosso amehukumiwa na Kamati ya Masaa 72 bila hata kusikiliza utetezi wake, tunaamini pia ufumbuzi utapatikana.”

Kwa upande wa Nyosso alisema; “Hii ni adhabu kubwa, imeniumiza na kuharibu maisha yangu, sasa nasubiri huruma yao baada ya kupeleka barua hiyo,”

Mwanaspoti ilimtafuta Katibu Mkuu wa TFF, Celestine Mwesigwa ambaye ilielezwa kuwa barua hiyo ilielekezwa kwake lakini simu yake alipopigwa iliita pasipo kupokelewa.
Credit:Mwanaspots


No comments: