Advertisements

Wednesday, September 21, 2016

AJALI YAUA 13 MWANZA

WATU 13 wamekufa na wengine 11 kujeruhiwa baada ya magari mawili ya abiria kugongana katika eneo la Mwamaya Wilayani Kwimba mkoani Mwanza leo asubuhi.
Akizungumza na Habarileo Mtandaoni, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, Ahmed Msangi alithibitisha kutokea ajali hiyo na kusema imetokea saa 12:15 asubuhi na ilihusisha gari dogo la abiria aina ya Toyota Hiace lenye namba za usajili T368 CWQ lililokuwa likotokea kijiji cha Shirima kwenda Mwanza mjini na basi aina ya Scania lenye namba za usajili T874 CWE.
Kamanda Msangi amesema ajali hiyo ilitokea wakati gari hilo dogo likiingia katika barabara kuu na kugongana na basi lililokuwa likitokea Mbeya kwenda Mwanza na kusababisha vifo na majeruhi waliokuwa katika gari dogo.
“Nipo njiani naenda eneo la tukio lakini taarifa za awali nilizopokea ni kuwa watu 13 wamefariki duniani na wengine 11 wamejeruhiwa na kati ya hao marehemu wawili ni watoto wadogo, na ajali imetokea katika makutano ya barabara kuu na hiyo kutokea kijiji cha Shirima ilipokuwa ikitokea gari ndogo."

No comments: