Advertisements

Tuesday, November 15, 2016

BALOZI SEIF AWATAKA MAWAZIRI KUORODHESHA CHANGAMOTO ZA MUUNGANO

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi akikiongoza Kikao cha Mawaziri, Manaibu Mawazini na Makatibu Wakuu wa SMZ kupokea mambo na utekelezaji wake yaliyokubalika kutekelezwa katika Vikao vya Kamati ya pamoja ya SMT na SMZ kuhusu kero za Muungano.
Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Nd. Joseph Abdulla Meza akiwasilisha Taarifa kwenye Kikao cha Mawaziri, Manaibu Mawazini na Makatibu Wakuu wa SMZ kuhusu kero za Muungano.

Baadhi ya Mawaziri, Manaibu Mawaziri na Makatibu Wakuu wa Wizara za SMZ wakiwa katika Kikao cha kupokea mambo na utekelezaji wake yaliyokubalika kutekelezwa katika Vikao vya Kamati ya pamoja ya SMT na SMZ kuhusu kero za Muungano.

                              Picha na – OMPR – ZNZ.
 


Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi ameziagiza Wizara za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kupitia Mawaziri, Watendaji Wakuu pamoja na Wataalamu wao kufanya uchambuzi wa kuorodhesha mambo ambayo yanaonekana kuleta changamoto kuhusu kero za Muungano.

Alisema orodha ya uchambuzi huo katika kila Sekta baadaye unapaswa kuwasilishwa katika Kamati ya Sekriterieti ya Vikao hivyo iliyo chini ya Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar.

Balozi Seif Ali Iddi alisema hayo wakati akikiongoza Kikao cha Mawaziri, Manaibu Mawaziri pamoja na Makatibu Wakuu wa Wizara za SMZ kilichofanyika Ofisini kwake Vuga Mjini Zanzibar kupokea mambo ambayo tayari yamekubalika kutekelezwa katika Vikao vya Kamati ya pamoja ya SMT na SMZ kuhusu kero za Muungano.

Alisema kazi iliyopo hivi sasa kwa Watendaji wa Kamati hiyo ya pamoja kwa upande wa Zanzibar ni kukumbushana kwa nia ya kutafuta mapungufu yaliyojitokeza ndani ya utekelezaji wa kero za Muungano hasa ikizingatiwa zaidi mabadiliko ya Uongozi yaliyojitokeza ndani ya Wizara za Serikali.

Naye Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mh. Mohammed Aboud Mohammed alieleza kwamba suala lolote wanalolihisi Mawaziri hao linafaa kuwa agenda ni vyema likawasilishwa mapema kwenye Kamati ya Sekriterieti.

Waziri Aboud alisema hatua hiyo itawapa fursa Watendaji wa Sekriteriet hiyo kuyapitia masuala hayo na kuyapa upendeleo wa kuingizwa katika agenda za Vikao vinavyotarajiwa kushirikisha Wajumbe wa Kamati ya Pamoja na pande hizo mbili.

Mapema akitoa Taarifa ya Kikao hicho Katibu wa Kamati ya Sekriteriet ya Kero za Muungamo ambae pia ni Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Nd. Joseph Abdulla Meza alisema Kamati hiyo tayari imeshafanya tathmini ya vikao vilivyopita.

Katibu Mkuu Meza alisema uchambuzi wa tathmini hiyo utaweza kuwasaidia Wajumbe wapya wa Kamati hiyo katika kujadili kwa kina masuala yanayohusu Changamoto za Muungano.

Wakichangia agenda hizo baadhi ya Washiriki wa Kikao hicho walipendekeza kuwepo kwa uelewa wa pamoja wa Washiriki hao katika kujadili masuala ya changamoto za Muungano ambao ndio njia rahisi ya upatikanaji wa ufanisi wa haraka.

Kikao cha Mwisho cha Kamati ya pamoja ya Mawaziri na Makatibu Wakuu wa Serikali ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar cha kujadili Kero za Muungano chini ya Mwenyekiti wake Makamu wa Rais wa Muungano kilifanyika Mjini Dodoma Mnamo Tarehe 23 Juni mwaka 2013.

Othman Khamis Ame

Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar

15/11/2016.


No comments: