Tuesday, January 3, 2017

BUNGE AITAKA SERIKALI KUWASAIDIA WANANCHI KUPATA MAJI

NaMussa Mbeho,Katavi

MBUNGE wa jimbo la Nsimbo Mkoani Katavi Mh.Richard Philipo Mbogo ameitaka serikali kupitia upya maamuzi ya kuvunja vizibo vinavyoingiza maji katika mashamba ya wakulima wa kata za Itenka,Mwamkulu na Katuma ili kuwasaidia kupata maji ya kutosha kumwagilia mazao yao baada ya vizibo vinavyosambaza maji kubomolewa.

Mbunge huyo ametoa ombi hilo leo katika mkutano wa hadhara uliofanyika katika kijiji cha Itenka B kilichopo kata ya Itenka Halmashauri ya Wilaya ya Nsimbo mkoani hapa ikiwa ni mwendelezo wa ziara yake ya kutembelea na kupokea kero za wananchi wa jimbo hilo.

Mh.Mbogo amesema kutokana na kubomolewa kwa vizibo hivyo katika kata hizo hali ya mazao imekuwa mbaya kwani maji yamekuwa hayafiki katika mshamba ya mpunga kutokana na zao hilo kutegemea sana maji kutoka katika vizibo hivyo alimaarufu kama kingo za maji yanayotoka katika mto katuma

Aidha ameongeza kuwa katika ,vikao vinavyotarajiwa kufanyika wiki ijayo serikali inapaswa kujadili namna ya kuwasaidia wakulima wa zao la mpunga katika kata za Mwamkulu,Itenka na Katuma ili kuwanusuru wakulima zaidi 20,000 wanaoishi kwa kutegemea kilimo cha zao la Mpunga.

Mh.Mbogo ametoa wito kwa wananchi kuendelea kutunza mazingira ikiwemo kuzingatia maelekezo ya serikali ya kutokutengeneza vizibo vingine wakati wakiendelea kulitafutia ufumbuzi suala hilo ili kuendelea kuhifadhi vyanzo vya maji visikauke.

Nao baadhi ya wananchi wa kata hizo ambao hawakupenda majina yao yatajwe gazetini wamesema kuwa mbali na kubomolewa kwa vizibo hivyo lakini pia wanakabiliwa na changamoto mbalimbali ikiwemo ukosefu wa maji safi na salama,zahanati,shule ya sekondari pamoja na miundombinu ya barabara kuwa mibovu hali ambayo inarudisha nyuma maendeleo yao.

Kwa upande wao viongozi wa chama cha mapinduzi ccm wilaya yam panda wakiongozwa na Mwenyekiti wake Bw.Beda Katani wamesema kuwa wamesikitishwa na maamuzi ya serikali ya kubomoa vizibo hivyo ambavyo vilikuwa tegemezi kwa wananchi wa kata hizo katika kuzarisha zao la mpunga.

No comments: