Advertisements

Friday, January 20, 2017

Jeshi la Senegal Laingia Gambia Kukabiliana na Rais Jammeh Aliyegoma Kuondoka Madarakani

GAMBIA: Vikosi vya majeshi kutoka nchini Senegal vimethibitisha kuingia katika ardhi ya Gambia katika muda ambao rais mpya Adama Barrow alipokuwa akiapishwa kwa lengo la kumuondoa madarakani Rais Jammeh aliyeng’ang’ania uatawala baada ya kushindwa uchaguzi.
Msemaji wa Jeshi la Senegal Kanali Abdou Ndiaye amethibitisha kwamba vikosi hivyo vimevuka mpaka na kupiga hatua kuelekea katika Mji Mkuu wa nchi hiyo, Banjul na kusema kwamba vikosi hivyo mpaka sasa havijakabiliana na ukinzani wa aina yoyote ingawa viliweka bayana kwamba vilikuwa vimejizatiti kwa mapigano ikibidi.

Mapema Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa inasemekana kwa siri limekuwa likiunga mkono juhudi za vikosi vya ECOWAS, kuhakikisha kwamba rais Barrow anachukua madaraka kutoka kwa rais aliyemaliza muda wake Yahya Jammeh. Rais huyo wa zamani wa Gambia, awali aligoma kuachilia madaraka.
Rais wa sasa Adama Barrow ameapishwa leo katika nchini jirani kwenye ubalozi wa Gambia ulioko mjini Dakar nchini Senegal na kufuatiwa na shamra shamra ubalozini hapo.
Mpaka sasa haijafahamika wazi lini rais mpya wa Gambia ataweza kurejea nchini mwake na kuchukua hatamu za uongozi kwa mara ya kwanza akiwa rais.
GPL

No comments: