Advertisements

Thursday, January 12, 2017

Nape ampongeza Diamond kutumbuiza Afcon

Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Nape Nnauye (kushoto) akimkabidhi bendera ya Taifa, Diamond Platnumz katika hafla ya kumuaga iliyofanyika Dar es Salaam jana. Msanii huyo anakwenda Gabon kutumbuiza ufunguzi wa mashindano ya Afcon yatakayoanza keshokutwa. Kulia ni Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa MultiChoice-Tanzania, Salum Salum na mchekeshaji Joti. (Picha na Cosmas Mlekani).
WAZIRI wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Nape Nnauye amempongeza mwanamuziki wa Tanzania, Nassib Abdul ‘Diamond Platnumz’ kwa kupata nafasi ya kutumbuiza kwenye ufunguzi wa fainali za Mataifa ya Afrika, Afcon.

Michuano hiyo itakayofanyika Gabon inatarajiwa kuanza keshokutwa hadi Februari 5 mwaka huu ambapo mataifa 16 yatashiriki.

Nape akizungumza katika hafla ya kumkabidhi bendera ya taifa Diamond Dar es Salaam jana, alisema kitendo cha msanii huyo kwenda kutumbuiza katika ufunguzi huo ni heshima kubwa kwa Tanzania.

Alimtaka Diamond kwenda kuliwakilisha vizuri taifa licha ya timu ya taifa ya Tanzania, Taifa Stars, kutopata nafasi ya kushiriki fainali hizo.


Nape pia aliishukuru Multi- Choice-Tanzania kwa kukubali kuwapatia tiketi sita wasanii wa Diamond ili kwenda kunogesha shoo hiyo ya mwanamuziki huyo mwenye mafanikio makubwa nchini.

Alisema nafasi ya Diamond angeweza kupewa msanii mwingine yeyote nyota kutoka katika nchi zinazojiita mahiri katika tasnia hiyo, na badala yake amepewa Mtanzania huyo.

Alisema hiyo ni fursa kubwa kwa Diamond kuitangaza Tanzania kimataifa katika muziki. Naye Diamond alimshukuru Nape kwa kupiga hodi MultiChoice na kuwaombea tiketi wasanii wake.

Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa MultiChoice- Tanzania, Salum Salum alisema Afcon ni uhondo mwingine kwa Watanzania kwani DStv ndio chaneli pekee itakayoonesha fainali hizo.

“DStv ndio itakuwa chaneli pekee yenye ruksa ya kuonesha fainali hizo za Afcon na TV nyingine yeyote ikionesha hapa nchini itakuwa inaiba matangazo,” alisema Salum.

Wiki iliyopita Diamond alipata fursa ya kutumbuiza wakati wa utoaji wa tuzo za wachezaji bora wa mwaka wa Afrika zilizoandaliwa na Shirikisho la Soka la Afrika (Caf) zilizofanyika Abuja, Nigeria.

Katika uzinduzi huo, Diamond ataimba kibao maalumu pamoja na wasanii Mohombi na Franco, kibao ambacho pia kitakuwa wimbo maalumu wa mashindano hayo.

HABARI LEO

No comments: