Advertisements

Thursday, March 16, 2017

NDEGE KUBWA YA KISASA YAANZISHA SAFARI ZANZIBAR

UJIO wa ndege ya kisasa aina ya Airbus 350 XWB ya Shirika la Ndege la Ethiopia `Ethiopian Airlines’ kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Abeid Amani Karume unatajwa ni miongoni mwa juhudi za kuimarisha sekta ya utalii na kuingiza mapato zaidi.

Ofisa Mwandamizi wa shirika hilo la ndege aliyepo Zanzibar, Eshetu Fikadu alisema hayo muda mfupi baada ya kutua kwa ndege hiyo yenye uwezo wa kubeba abiria 315.

Alisema kuwasili kwa ndege hiyo ya kisasa ni sehemu za juhudi za shirika hilo kupanua huduma zake na kufanya safari za uhakika kwa kutumia ndege kubwa.

Alisema kuanza safari kwa ndege hiyo ni miongoni mwa ndoto zao kutoa huduma zake kwa kutumia ndege zenye hadhi na teknolojia ya kisasa inayokwenda na wakati.

“Hayo ndiyo malengo yetu ambayo tumeyafikia kwa sasa kuhakikisha tunatoa huduma zinazokubalika na kwenda na wakati kwa kukidhi mahitaji ya abiria,” alieleza.

Baadhi ya watu waliohojiwa, walisema ujio wa ndege hiyo ya kisasa kwa kiasi kikubwa utasaidia kuimarika kwa sekta ya utalii na malengo yake kwa ajili ya kuimarisha uchumi.

Mwenyekiti wa Kampuni inayotoa huduma za usafiri wa anga kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Abeid Amani Karume (ZATI), Mohamed Raza alisema ujio wa ndege ya shirika hilo unakwenda sambamba na malengo ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ifikapo mwaka 2020 kuhakikisha inapokea zaidi ya watalii 500,000.

Ofisa Mwandamizi wa uwanja huo, Zaina Mwalukuta alisema huduma za uwanja huo zimeimarika na kufikia kiwango cha kimataifa.

HABARI LEO

No comments: