Advertisements

Thursday, April 20, 2017

MAKAMU WA RAIS MHE. SAMIA AFANYA MAZUNGUMZO NA KAMISHNA MKUU WA TRA

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akizungumza na Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato nchini (TRA) Bw. Charles Kichere (kushoto) aliyemtembelea leo ofisini kwake, Ikulu jijini Dar es Salaam.
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akizungumza na Kamishna Mkuu wa TRA Bw. Charles Kichere (kushoto)ambaye aliongozana na Mkurugenzi wa Elimu ya Mlipa Kodi TRA Bw. Richard Kayombo (kushoto), Ikulu jijini Dar es Salaam.
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akizungumza na Afisa Mahusiano Mwandamizi wa Mamlaka ya Mapato (TRA)Tanzania Bi. Mariamu Mwayela mara baada ya kumaliza mazungumzo yake na Kamishna Mkuu wa Mamlaka hiyo Bw. Charles Kichere.


Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe Samia Suluhu Hassan amemwagiza Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Charles Kichere ahakikishe anaweka utaratibu wa kukutana na wafanyabiashara mara kwa mara kama njia ya kujadili na kutatua kero mbalimbali zinazowakabili wafanyabiashara hao.

Makamu wa Rais Mhe Samia Suluhu Hassan amesema hayo alipokutana na kufanya mazungumzo na Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Charles Kichere kuhusu namna bora ya kutatua kero mbalimbali zinazowakabili wafanyabiashara nchini kama hatua ya kuongeza kasi ya ukusanyaji wa kodi wa kwa ajili ya maendeleo ya Taifa.

Makamu wa Rais ameonyesha kusikitishwa na baadhi ya Maafisa wa TRA kuwanyanyasa wafanyabiashara na wengine kuwabambikizia kodi kubwa hali ambayo inazua malalamiko mengi kutoka kwa wafanyabiashara hao jambo ambalo amesema ni muhimu likatafutiwa ufumbuzi haraka iwezekanavyo.

Amesisitiza kuwa ni muhimu kama TRA itafanya mabadiliko yeyote ya ulipaji wa kodi ikawafahamisha wafanyabiashara hao mapema ili kuondoa usumbufu mkubwa unaoweza kutokea katika ulipaji wa kodi pindi wanapoagiza bidhaa mbalimbali kutoka nje ya nchi.

Makamu wa Rais amesema lengo la Serikali ni kuhakikisha ulipaji wa kodi kwa ajili ya maendeleo ya Taifa unafanyika kwa kuzingatia kanuni, sheria na taratibu na sio kuwakandamiza Watanzania kwa kuwalipiza kodi mara mbili jambo ambalo amesema halifai hata kidogo.

Makamu wa Rais amemtaka Kamishna wa TRA kukomesha mara Moja tabia ya baadhi ya Maafisa wa mamlaka hiyo kutoa lugha chafu na kuudhi kwa wafanyabiashara bali watumie lugha nzuri ili kuhamasisha wafanyabiashara kulipa kodi kwa hiyari bila kulazimishwa na mtu.

Makamu wa Rais pia ameipongeza TRA kwa kazi kubwa inayoifanya katika ukusanyaji wa mapato na amewapa moyo wa kuongeza bidii katika ukusanyaji wa kodi hizo ambazo Serikali inatumia katika ujenzi wa miundombinu mbalimbali nchini.

Kwa upande wake, Kamishna Mkuu wa TRA nchini Charles Kichere amemuahidi Makamu wa Rais kuwa atafanya kazi kwa bidii ili kuhakikisha malalamiko mbalimbali yanayotolewa na Wafanyabiashara yanapata ufumbuzi haraka iwezekanavyo.

Kamishna Kichere amesisitiza kuwa kwa baadhi ya maafisa wa Mamlaka hiyo wanaokiuka maadili ya kazi ataendelea kuwachukulia hatua stahiki ili kurejesha nidhamu katika utendaji wa kazi na ukusanyaji wa mapato.

No comments: