Advertisements

Wednesday, May 10, 2017

ASASI ZA KIRAIA ZASAIDIA KUWAPA RAIA SAUTI

Majadiliano ya jumuiya katika kata ya Mpapula mkoani Mtwara, mwanajamii akielezea uzoefu wao kuhusu vitendo vya ukatili vinavyofanywa dhidi ya wanawake na watoto. Majadiliano hayo yaliandaliwa na asasi ya kiraia ya Wanasheria Wanawake Katika Maendeleo Afrika (Women in Law and Development in Africa - WiLDAF), mojawapo kati ya asasi za kiraia zilizopokea msaada kutoka mradi wa Pamoja Twajenga uliokuwa ukifadhiliwa na USAID. (Picha kwa hisani ya: Rhoda Nashon/WiLDAF)


Ubalozi wa Marekani
Dar es Salaam
TANZANIA
10 Mei, 2017
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

ASASI ZA KIRAIA ZASAIDIA KUWAPA RAIA SAUTI

Dar es Salaam, TANZANIA.  Taasisi na Asasi Zisizokuwa za Kiserikali za Tanzania (NGOs) taasisi za serikali zinazoshughulikia uwajibikaji na wadau wengine kadhaa walikutana hivi leo  ili kufanya tathmini ya hatua zilizopigwa na mafunzo yaliyopatikana wakati wa uhai wa mradi wa Pamoja Twajenga  unaofadhiliwa na Serikali ya Marekani kupitia Shirika la Marekani la Maendeleo ya Kimataifa (USAID). Toka mwaka 2013, watendaji wa mradi wa Pamoja Twajenga wamekuwa wakifanya kazi bega kwa bega na asasi za kiraia na taasisi za serikali ya Tanzania zinazoshughulikia masuala ya uwajibikaji ili kuimarisha mahusiano kati ya asasi za kiraia na serikali. Mradi huu ulitoa mafunzo na msaada kwa jumla ya asasi zisizo za Kiserikali 16 na taasisi tatu za serikali zinazojihusisha na uwajibikaji katika mikoa ya Mtwara, Iringa, Dodoma, Morogoro na  Zanzibar kwa lengo la kukuza uwazi na uwajibikaji wa serikali kwa raia wa Tanzania.


Kutokana na msaada huu, hivi sasa asasi za kiraia na taasisi za uwajibikaji zilizoshiriki zina uwezo zaidi wa kushiriki katika mijadala kuhusu masuala mahsusi yanayozigusa jamii (issue-based dialogue). Raia katika mikoa lengwa ya mradi – ikiwa ni ni pamoja na vijana, wanawake na makundi mengine ya watu wanaowekwa pembezoni wana uwezo zaidi wa kujadiliana na serikali zao kuhusu kero zao, jambo ambalo limeongeza uwajibikaji na uwazi katika usimamizi wa rasilimali za umma na katika ufanyaji maamuzi. Asasi za kiraia zilizosaidiwa na mradi wa Pamoja Twajenga zinafanya kazi katika masuala yanayohusiana moja kwa moja na mahitaji ya msingi ya raia ikiwa ni pamoja na huduma za afya, elimu, usalama wa chakula na usimamizi wa rasilimali.  

Mathalan, wanakijiji katika kijiji cha Kibaigwa, mkoani Dodoma walikuwa wakilazimika kwenda umbali wa kilomita 45 ili kupata kituo cha afya chenye huduma ya wodi ya wazazi. Asasi ya Kiraia iliyofadhiliwa na mradi huu itwayo TACOSODE,iliwasaidia wanakijiji hao kujadiliana na uongozi wa kijiji chao kuhusu haja ya kumalizia wodi mpya ya akinamama. Mjadala huo uliifanya kamati ya kijiji kuwasilisha katika serikali ya wilaya ombi la fedha kwa ajili ya kazi hiyo. Ujenzi wa wodi hiyo ulikamilika mwezi Oktoba 2015 na hivi sasa inahudumia jamii.

Asasi nyingine iliyosaidiwa na mradi wa Pamoja Twajenga ni Chama cha Wanasheria watetezi wa Mazingira (LEAT) ambayo ilitoa mafunzo ya usimamizi wa maliasili na uwajibikaji kwa jamii (social accountability) kwa kijiji cha Kiwere mkoani Iringa. Mafunzo haya yaliwawezesha wanakijiji kuchukua hatua ya kutaifisha mbao ambazo zilikuwa zimevunywa isivyo halali katika ardhi yao.

Kupitia misaada mbali mbali kwa asasi za Kiraia za Kitanzania na taasisi za serikali za uwajibikaji mradi wa Pamoja Twajenga  umesaidia kuimarisha mfumo wa majadiliano na ushiriki ambapo asasi zinaweza kupata matokeo makubwa na endelevu zikiwa kama asasi za ushawishi na utetezi katika sekta zao mahsusi.

Katika hotuba yake ya ufunguzi wa mkutano wa leo, Naibu Mkurugenzi wa USAID nchini Tanzania David Thompson alisisitiza, “mradi huu umejielekeza katika azma moja kuu iliyo rahisi kueleweka: kwamba mstakabali wa Tanzania unategemea ushiriki huru na imara wa raia kutoka katika nyanja zote za maisha. Nyote mliokusanyika hapa hivi leo, iwe mnawakilisha asasi za kiraia au Serikali ya Tanzania mmekuwa na mchango mkubwa katika kufikia azima hii. Asanteni kwa ubia wenu. Tanzania imechukua hatua muhimu katika kuinua uwazi, kuimarisha utoaji huduma za jamii, kuhakikisha kuwepo kwa nafasi ya kidemokrasia na kuwasaidia raia kuchagiza mabadiliko.”

Kwa taarifa zaidi, tafadhali wasiliana na Ofisi ya Habari ya Ubalozi wa Marekani Dar es Salaam kwa simu namba: +255 22 229-4000 au kwa barua pepe: DPO@state.gov.

No comments: