Advertisements

Friday, May 19, 2017

POLISI YATAJA MTANDAO WATUHUMIWA WA MAUAJI

Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Pwani, Onesmo Lyanga
JESHI la Polisi limeanza kuwasaka watuhumiwa 12 wa mauaji ya Polisi na raia katika wilaya za Mkuranga, Kibiti na Rufiji, mkoani Pwani, baada ya kuwabaini kutokana na vyanzo mbalimbali.

Aidha, katika kukoleza kasi ya msako huo, jeshi hilo limetangaza kutoa dau nono la Sh milioni 5 kwa watakaofanikisha kukamatwa kwa watuhumiwa hao. Hayo yalibainika jana mjini hapa kupitia taarifa iliyotolewa na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Pwani, Onesmo Lyanga.

Amewataja watuhumiwa hao kuwa ni pamoja na Abdulshakur Makeo aliyetajwa kuwa ni mwanzishi wa harakati za mauaji Ikwiriri, wilayani Rufiji. Wengine ni Faraj Nangalava, Anaf Kapera pia anafahamika zaidi kama Kapelo, Said Ngunde, Omar Matimbwa, Shaaban Kinyangulia, Haji Ulatule, Ally Ulatule, Hassan Uponda, Rashid Mtulula, Shehe Hassan Mzuzuri na Hassan Njame.

“Jeshi la Polisi mkoani Pwani limefanya jitihada kubwa kwa kushirikiana na wasiri wetu kuwabaini watuhumiwa wa vitendo vya mauaji vinavyoendelea katika mkoa wetu hususan wilaya za Kibiti, Rufiji na Mkuranga.

”Watuhumiwa hawa hupendelea kutembelea maeneo ya kisiwa cha Simbaulanga, kisiwa cha Saninga, Kijiji cha Nchinga, Kijiji cha Mfesini katika Kata ya Nyamisati na maeneo mbalimbali ya wilaya za Kibiti, Rufiji na Mkuranga,” alisema kamanda Lyanga.

Ametoa mwito kwa wananchi kutoa ushirikiano kwa siri ili kuweza kufanikisha kuwafichua watuhumiwa hao wanaohatarisha hali ya usalama mkoani Pwani, huku akisema zawadi ya Sh milioni 5 itatolewa kwa yeyote atakayefanikisha kupatikana kwa watuhumiwa hao wanaohusishwa pia na mauaji ya askari polisi wanane Aprili 13 mwaka huu katika kijiji cha Makengeni, Rufiji.

Aidha, katika matukio hayo ya mauaji yaliyoondoa pia uhai wa watu watatu Februari 21 mwaka huu akiwemo Mkuu wa Upelelezi Wilaya ya Kibiti, Peter Kubeza, inakadiriwa kwa ujumla karibu watu 31 wamepoteza maisha, wakiwemo viongozi na makada wa chama tawala, Chama Cha Mapinduzi (CCM).

Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mwigulu Nchemba akizungumza bungeni hivi karibuni alisema Serikali inalichukulia matukio hayo kwa uzito mkubwa ili kuhakikisha wanarejesha hali ya usalama katika maeneo hayo na nchi nzima.

Alitumia fursa hiyo kuwatoa hofu wananchi na kusema kuwa matukio hayo yameipa Serikali chachu zaidi ya kupambana na uhalifu katika kuhakikisha wananchi wanakuwa katika mazingira salama

HABARI LEO

No comments: