Advertisements

Saturday, June 3, 2017

WAZIRI MKUU AAGIZA KILOSA WAILIPE GAIRO DENI LA0

* Ni la sh. milioni 213/- la fedha za maendeleo.
*Ataka apewe taarifa ifikapo Juni 30.
          
WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amemwagiza Katibu Tawala wa Mkoa wa Morogoro, Bw. Clifford Tandari aitishe kikao na uongozi wa Halmashauri ya Kilosa na kupata kauli yao ni lini watalipa zaidi ya sh. milioni 210 wanazodaiwa na Halmashauri ya Gairo.

“Katibu Tawala itisha kikao cha Mwenyekiti wa Halmashauri, Mkuu wa Wilaya na Mkurugenzi wa Halmashauri, waseme ni lini watazileta fedha hizo ambazo zilitumwa kwao wakati Halmashauri ya Wilaya ya Gairo ikiwa haijafungua akaunti zake,” amesema.

Ametoa agizo hilo leo (Jumamosi, Juni 3, 2017) wakati akizungumza na viongozi wa mkoa wa Morogoro, wilaya ya Gairo na watumishi wa Halmashauri ya Gairo mara baada ya kupokea taarifa ya mkoa na wilaya katika kikao kilichofanyika Gairo mjini.

“Kilosa ni lazima wazilipe hizo fedha. Katibu Tawala simamia zoezi hilo na kama watachelewa, uzikate moja kwa moja kwenye fedha yao wanayoletwa kutoka Ofisi ya Rais (TAMISEMI). Nataka nipewe taarifa ya maamuzi hayo kabla Juni haijaisha,” amesema.



Mapema akitoa taarifa ya wilaya hiyo, Mkuu wa Wilaya ya Gairo, Bi. Siriel Mchembe alisema wanaidai Halmashauri ya Kilosa sh. 233,228,679 ambazo ziliingizwa huko wakati wilaya hiyo  inaanzishwa na hawakuwa wamefungua akaunti ya wilaya.

“Fedha hizi zilikuwa zinapitia Kilosa wakati wilaya ya Gairo imeanzishwa kwa kuwa kipindi hicho wilaya ya Gairo ilikuwa bado haijafungua akaunti. Fedha hizi zinajumuisha ruzuku ya uendeshaji, mapato ya ndani na miradi ya maendeleo,” alisema.

Alisema Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) iliagiza wilaya ya Kilosa ilipe deni hilo kabla ya Juni 2016 lakini hadi sasa wameshalipa sh. milioni 20 tu ambapo sh. milioni 10 zililipwa Desemba 2015 na nyingine milioni 10 zililipwa Mei 2017.

Akisisitiza kuhusu makusanyo ya mapato, Waziri Mkuu amewakumbusha watumishi hao kuwa Serikali imekwishatoa agizo la kutumia mashine za kielektroniki kukusanya mapato ifikapo Julai mosi.

“Makusanyo ya mapato ya ndani ni eneo muhimu sana. Tumeshaagiza, mwisho wa kutumia mifumo ya kawaida ni Juni 30. Kuanzia Julai mosi, kila eneo ni lazima litumie mashine za kielektroniki,” alisema Waziri Mkuu.

Alihoji ni kwa nini Halmashauri ya Gairo ililenga kukusanya sh.milioni 889.5 lakini kufikia Aprili mwaka huu, makusanyo halisi yalikuwa ni sh. milioni 356.2 sawa na asilimia 40.

Alitumia fursa hiyo kuwapongeza Mamlaka ya Mapato (TRA) ya wilaya hiyo ambao hadi kufikia Aprili, 2017 wameweza kukusanya sh. milioni 601.5 ikilinganishwa na makadirio yao ya kukusanya sh. milioni 471 kwa mwaka. Waziri Mkuu aliwapongeza kwa sababu wamevuka lengo kwa asilimia 127.6.

Waziri Mkuu ambaye yuko kwenye ziara ya siku ya wilaya hiyo, asubuhi alipanda mti kwenye Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ikiwa maadhimisho ya siku ya upandaji miti hapa nchini.

Pia alikagua mradi wa maji wa kijiji cha Chakwale, na mradi wa visima 10 ambayo imekuwa na mgogoro kwa muda mrefu. Pia atazungumza na wananchi wa Gairo mjini kwenye mkutano wa hadhara.

No comments: