Advertisements

Saturday, July 8, 2017

JKCI Yakaribisha Wananchi Kupima Afya Bure

  Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) Profesa Mohamed Janabi akiteta jambo na baadhi ya wafanyakazi wa Taasisi yake alipotembelea Maonesho ya 41 ya Kimataifa ya Biashara Dar es Salaam. Kushoto ni Afisa Uhusiano wa Taasisi hiyo Bi. Anna Nkinda.
 Daktari Bingwa wa Upasuaji wa Moyo wa Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI), Dkt. Bashir Nyangasa akielezea namna upasuaji wa moyo unavyofanywa kwa mmoja wa mwananchi aliyetembelea banda la taasisi hiyo katika Maonesho ya 41 ya Kimataifa ya Biashara Dar es Salaam (Sabasaba).
 Wananchi wakipata huduma ya vipimo katika banda la Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) wakati wa Maonesho ya 41 ya Kimataifa ya Biashara Dar es Salaam (DITF).

Frank Mvungi- Maelezo
Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete imewataka Wananchi  kujitokeza kwa wingi kupima afya zao hasa magonjwa ya moyo katika msimu huu wa maonesho ya Kimataifa ya 41 ya Biashara ya Dar es Salaam yanayofanyika katika viwanja vya JK Nyerere jijini Dar es Salaam.
Akizungumza katika viwanja vya maonesho hayo Mkurugenzi Mkuu  wa Taasisi hiyo Prof. Mohamed Janabi amesema kumekuwa na muitikio mkubwa sana kwa wananchi kutembelea banda lao ambapo amesema kuwa kwa siku takribani watu 700 wanafika katika banda hilo kwa ajili ya kupata huduma na ushauri.
“Ni vizuri watanzania wakatumia fursa hii kufika hapa  na watapatiwa baadhi ya vipimo na ushauri  bure katika banda  letu lililopo ndani ya viwanja vya sabasaba kwa kuwa dhamira ya Serikali ya Awamu ya Tano ni kuwahudumia wananchi wake kwa kuhakikisha kuwa wanapata huduma zote za msingi zenye kiwango na ubora,” Alisisitiza Prof. Janabi
Akifafanua  Prof. Janabi amesema  Taasisi hiyo imedhamiria kuwahudumia wananchi wakati wote wa maonesho na hata baada ya hapo wapo tayari kuwahudumia wale wanaohitaji huduma katika taasisi hiyo.
Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete imekuwa ikitoa huduma za upasuaji wa moyo tangu kuanzishwa kwake hali inayosaidia kupunguza gharama zilizokuwa zinatumika kusafirisha wagonjwa kwenda nje ya nchi kwa matibabu kwa kipindi kirefu sasa.

No comments: