Advertisements

Monday, July 10, 2017

Muhimbili yawezesha watoto kusikia kwa mara ya kwanza


 Muwakilishi wa Medel Afrika Mohamed El Disouky akimfanyia mazoezi ya kuzungumza mtoto Asma Athuman Mwinyi ambaye alipata matatizo ya kusikia akiwa na miaka sita.
Mtaalam Mohamed El Disouky akimfanyia majaribio ya kifaa cha usikivu mtoto Silas Machaku ( 3 ) ambaye aliwekewa kifaa maalum cha usikivu kwa ndani (Internal complete) lakini leo amewekewa kifaa kwa nje (External complete) ili aweze kusikia . zoezi hilo limefanyika katika Hospitali ya Taifa Muhimbili.


Watoto watano waliofanyiwa upasuaji na kuwekewa vifaa maalum  vya kusaidia kusikia (Cochlear Implant) leo wamewashiwa vifaa hivyo ili waweze kusikia kwa mara ya kwanza.
Zoezi hilo  limefanywa leo na wataalam wa Hospitali ya Taifa Muhimbili kwa kushirikiana na watalaam kutoka MEDEL .
Daktari Bingwa wa magonjwa ya Masikio, Pua na Koo Edwin  Liyombo amesema Juni   5 na 6 mwaka huu watoto hao walifanyiwa upasuaji huo kwa mara ya kwanza na kuwekewa vifaa maalum kwa ajili ya kusikia (Internal complete) lakini leo wamekuja kuwekewa na  kuwashiwa  vifaa vya nje(External complete) ili waweze kusikia.
Kwa upande wake mtaalam wa vifaa vya usikivu Fayaz Jaffer amesema baada ya kuwekewa kifaa hivyo watoto hao wanapaswa kurudi kila baada ya wiki mbili kwa miezi mitatu na baada ya hapo  watarudi  wiki mbili kwa miezi sita ili kufanyiwa mazoezi.
‘’Baada ya hapo wanaanza kuwafanyia mazoezi ya kuongea ( speech therapy) ndani ya mwaka mmoja na kadiri umri unavyozidi kwenda watakuwa wameshaanza kusikia na kujifunza kuongea na kupelekwa kujifunza zaidi katika shule za kawaida na si shule maalum kama ilivyozoeleka” amesema mtaalam huyo.
Juni 7 mwaka huu Waziri wa Afya Maendeleo ya Jamii, Jinsia , Wazee na Watoto Ummy Mwalimu alizindua huduma ya upasuaji wa kupandikizaji wa vifaa vya usikivu katika Hospitali ya Taifa Muhimbili , ambapo katika Hospitali za Umma Tanzania imekuwa nchi ya kwanza kutoa huduma hiyo  na ya pili katika nchi za Ukanda wa Afrika Mashariki ikitanguliwa na Kenya.

No comments: