Advertisements

Friday, August 4, 2017

Bunduki 395 na risasi 1478 zakamatwa kwa kipindi cha mwaka mmoja kupitia doria za ujangili nchini.

Jumla ya bunduki 395 na risasi 1478 na magazine mbili zimekamatwa kwa kipindi cha mwaka mmoja kupitia doria za kukabiliana na ujangili zinazofanywa na wizara ya maliasili na utalii katika hifadhi za taifa na mapori ya akiba nchini huku watuhumiwa 472 wakifungwa vifungo virefu jela kwa ujangili na wengine 469 wakitozwa faini ya zaidi ya shilingi milioni 452.
Akitoa taarifa ya utendaji wa wizara hiyo waziri wa maliasili na utalii Profesa Jumanne Maghembe anasema mafanikio hayo yanatokana na doria laki tatu na nusu zilizofanyika nchi nzima ambapo mauaji ya Tembo yamepungua kwa asilimia 45 huku changamoto kubwa ambayo bado inaikabili sekta hiyo ni uingizwaji wa mifugo kwenye maeneo yaliyohifadhiwa.

Kuhusu utalii waziri Maghembe anasema unakuwa kwa wastani wa asilimia 12 kwa mwaka huku idadi ya watalii ikizidi kuongezeka ambapo kwa mwaka 2016 mapato ya sekta hiyo yakiongezeka na kufikia dola za kimarekani bilioni 2.1 ikilinganishwa na dola bilioni 1.9 kwa mwaka 2015.

Twaha twaibu ni afisa uhusiano wa mamlaka ya usimamizi wa wanyamapori nchini tawa ambaye anasema kwa kipindi kifupi tangu mamlaka hiyo kuanza kusimamia sekta ya wanyamapori matukio ya uijangili yamepungua huku ikolojia ikionyesha idadi ya wanyama kuongezeka.

No comments: