Advertisements

Sunday, August 6, 2017

Wajumbe Bodi Umwagiliaji kukamatwa

MKUU wa Wilaya ya Kilombero, James Ihunyo ameagiza kukamatwa kwa Wajumbe wa Bodi ya Skimu ya Umwagiliaji ya Mkula kutokana na kuchelewesha kwa makusudi malipo ya mkopo walioupata kutoka Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB).

Akizungumza wakati wa mkutano wa pamoja na wanachama wa skimu hiyo, Ihunyo alisema uzembe wa bodi hiyo umesababisha kuchelewesha marejesho ya mkopo wa takribani Sh milioni 790. Aliongeza kuwa, kitendo cha bodi hiyo kinarudisha nyuma juhudi za serikali katika kupambana na umasikini nchini.

Alisema kuchelewesha kurudisha mikopo hiyo kunakosesha wakulima wengine kuchelewa kupata fursa hizo za mikopo hiyo nafuu inayotolewa na TADB ambayo imelenga kuchagiza na kusaidia mapinduzi ya kilimo kutoka kilimo cha kujikimu kwenda cha kibiashara ili kuchangia kwenye ukuaji wa uchumi na kupunguza umasikini.

Akizungumza katika mkutano huo, Mwakilishi wa Kaimu Mkurugenzi Mtendaji, Adam Kamanda alisema tangu wapatiwe mkopo huo, baadhi ya wakulima wa skimu hiyo wamekuwa wakichelewesha kwa makusudi kurejesha mkopo huo licha ya jitahada za kuwahimiza kurejesha mkopo huo.

Kamanda aliongeza kuwa benki ya kilimo imejipanga kuhakikisha inatekeleza maelekezo ya serikali ya kuwawezesha wakulima nchini katika sekta ya kilimo kwa kusaidia upatikanaji na utoaji wa fedha ikiwa ni pamoja sera nzuri zitakazosaidia maendeleo ya kilimo.

HABARI LEO

No comments: