Advertisements

Thursday, September 21, 2017

Madaktari wazuia Lissu kusafirishwa Marekani

By Mwandishi Wetu, Mwananchi

Dar es Salaam. Mbunge wa Singida Kaskazini(CCM), Lazaro Nyalandu amesema kwamba madaktari wa Kenya wamesema Tundu Lissu hawezi kusafirishwa kwenda nje kwa ajili ya kumpatiwa matibabu.

Mbunge Nyalandu ameeleza hayo kwenye ukurasa wake wa Instagram, Facebook na Twitter kwamba mipango ya kumsafirisha Lissu ambayo walikuwa wanafanya itasimama kwa sasa kutokana na ushauri wa madaktari hao ili kuruhusu kukamilishiwa huduma za tiba ambazo tayari ameanzishiwa, hadi hapo itakavyoshauriwa vinginevyo.

Katika kurasa zake hizo za mitandao ya kijamii Nyalandu ameandika hivi, “Tunafahamu kwamba, tangu Alhamisi, Septemba 7, siku ambayo Mh #TunduLissu, Mb., (Singida Mashariki-CHADEMA) alishambuliwa kwa kupigwa risasi mjini DODOMA, Watanzania wengi wamesononeshwa na kulia sana, na kubwa zaidi, WOTE wameungana katika kuomba Sala na Dua kwa ajili ya Mh #TunduLissu, ili mkono wa Mkombozi, aliye MUNGU wetu, upate kumgusa tena na kumponya dhidi ya majeraha, maumivu na mateso anayoyapitia,”

“Mapema leo(jana), baada ya kutembelea #Nairobi Hospital asubuhi, nimefanya mazungumzo mchana wa leo na Mh #FreemanMbowe, ambapo kwa pamoja tumeelezwa kuwa MADAKTARI #NairobiHospital wameendelea na kumtibu Mh #TunduLissu, ikiwa ni pamoja na kuanza upasuaji, na huduma zingine za Kitabibu walizomwanzishia tangu awasili Nairobi siku ya Alhamisi, Septemba 7. IMEELEZWA vilevile kuwa kwa sasa Mh #TunduLissu ataendelea na TIBA hospitalini hapo kutokana na kile kilichoelezwa kuwa hali yake bado ni "Critical but stable", na KWAMBA mwili wake unaendelea kuitikia vema matibabu lukuki anayofanyiwa kwa wakati mmoja,”

“KWA SASA, mipango ya kumsafirisha Mh #TunduLissu NJE itasimama, kutokana na ushauri wa MADAKTARI #NairobiHospital, ili kuruhusu kukamilishiwa huduma za TIBA ambazo tayari ameanzishiwa, hadi hapo itakavyoshauriwa vinginevyo, ama endapo kutatokea umuhimu wa kufanya hivyo katika SIKU zijazo,”

“AIDHA, SOTE tuzidi KUMWOMBEA MUNGU na kushiriki katika CHANGIZO za kusaidia gharama za matibabu yake,”

“NI DHAHIRI kwamba Wana Singida, na Watanzania WOTE tumeumia, tumekwazwa, na tumesononeshwa sana kwa uonevu na dhuluma aliyotendewa ndugu yetu Mh #TunduLissu. Kitendo hiki hakikubaliki mbele za MUNGU na mbele za wanadamu,”

“Tunaiomba Serikali yetu iendeleze juhudi zake na kuchukua hatua za haraka kuwasaka, kuwakamata, na kuwatia mbaroni watu wote waliohusika kupanga na kutekeleza shambulio hili la kigaidi dhidi ya Mh #TunduLissu. Aidha, shambulio hilo walilolifanya watu wasiojulikana limedhalilisha taifa, na kudhoofisha taswira ya kukomaa kwa demokrasia inayoruhusu kuvumiliana na kuheshimiana licha ya tofauti zetu za kiitikadi na mitazamo ya kisiasa,”

“HALIKADHALIKA, kwetu sote kama TAIFA, huu ni wakati wa Watanzania wote kuwa wamoja, bila kujali tofauti zetu za kiitikadi, kidini, wala kikabila, tuungane na kulaani kitendo hiki na vitendo vyote vya uonevu na kuumizana. TANGU zamani, IMEANDIKWA: Haki HUINUA Taifa.”

No comments: