Advertisements

Saturday, January 13, 2018

AHUKUMIWA MIAKA MITATU JELA KWA KUMTUSI NA KUMTISHA MKUU WA WILAYA

Mahakama ya Wilaya ya Igunga mkoani Tabora, imemhukumu mkazi wa mtaa wa barabara ya Mbutu, mjini hapa, Mohamed Ahmed (54) kifungo cha miaka mitatu jela baada ya kutiwa hatiani kwa kumtishia na kumtolea lugha ya matusi Mkuu wa Wilaya ya Igunga, John Mwaipopo.

Mwendesha Mashtaka wa Polisi, Elimajidi Kweyamba, alidai mahakamani hapo kwamba mshitakiwa, alitenda kosa hilo Januari 09, mwaka huu, saa 1:05 usiku katika maeneo ya barabara kuu ya lami ya Igunga mjini.

Alidai kuwa mshitakiwa huyo alimtolea lugha ya matusi Mwaipopo wakati akitekeleza majukumu yake.

Mbele ya Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Wilaya ya Igunga, Ajali Milanzi, Kweyamba alidai kuwa mshtakiwa alitenda kosa hilo wakati mkuu wa wilaya akitekeleza agizo la upandaji miti kama lilivyotolewa maelekezo na Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassani.

Aidha, mwendesha mashtaka alidai kwamba katika kosa la pili, muda huo huo na tarehe hiyo hiyo, mshitakiwa akiwa na nia ovu, alimtishia maisha kwa maneno Mkuu wa Wilaya kuwa atamwonyesha na atahakikisha anahama Igunga kwa kumfanyia kitu kibaya.


Hata hivyo, baada ya kusomewa mashitaka yote mawili, mshtakiwa huyo alikiri kutenda makosa hayo.

Kabla ya kutoa hukumu, Hakimu Milanzi alisema kwa kuwa mshtakiwa amekiri mwenyewe makosa, atatumikia adhabu ya kifungo cha miaka mitatu gerezani, mwaka mmoja kwa kosa la kwanza na miwili kwa kosa la pili.

1 comment:

Anonymous said...

Mheshimiwa Hakimu Milanzi, I wish na Kesi nyingine zingekuwa mnaziendesha kwa kasi hii. Kosa limefanyika January 9 Leo Hukumu imeshatoka au kwa kuwa ni Versus Mkuu wa Wilaya.

Huwa najaribu kuangalia Mrundikano wa Watuhumiwa kwenye Mahabusu zetu, hali inatisha na inasikitisha sana.