Advertisements

Saturday, January 13, 2018

RC TABORA: AMCOS ZOTE KUANZA KUPANDA MITI JUMATATU

NA TIGANYA VINCENT
VIONGOZI wa vyama vya ushirika vya msingi (AMCOS) wameagizwa  kuhakikisha wanasimamia wanachama wao wanapanda miti ili   kuhifadhi mazingira na kupata nishati ya kukaushia tumbaku.
Kauli hiyo ilitolewa jana wilayani Urambo na Mkuu wa Mkoa wa Tabora Aggrey Mwanri wakati akitangaza wiki ya upandaji miti kwa ngazi ya AMCOS na wanachama wake.
Alisema kuwa kama wahitaji wa kuni za kukaushia tumbaku yao wanatakiwa kuhakikisha kuwa wanaungana na Serikali kutumia miundo mbinu walionayo kuhakikisha wanapanda miti katika maeneo na mashamba yoa ili zao hilo liwe endelevu.
Mkuu huyo wa Mkoa alisema kuwa Kampuni zinazonunua tumbaku mkoani humo zimekuwa zikiwapa wakulima miche za miti lakini baadhi ya Vyama vya Ushirika Vya Msingi vimekuwa vikiishia katika kuitupa chini ya miti mikubwa au vingine kuiacha katika Ofisi za vyama husika.
Mwanri alisema kuwa Ushirika ni chombo chenye nguvu na hivyo wakitumia nafasi walionayo watasaidia sana katika zoezi la upandaji miti mkoani Tabora kwa ajili ya kugeuza Tabora kuwa ya kijani na kuongeza kiwango cha mvua.
Alisema kuwa ili kuhakikisha kuwa wakulima hao wameitikia wito huo wataendesha zoezi la ukaguzi wa mashamba ya wakulima wa tumbaku ya miti na ya Ushirika yaliyopandwa mwaka huu ili kujiridhisha kama wametekeleza agizo hilo.
Naye Afisa Ushirika kutoka Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Tabora Fortunatus Mkoba aliwakumbusha wanaushirika kuwa wanatakiwa kila mkulima kuhakikisha kuwa anapanda miti 250 kwa kila ekari moja ya tumbaku anayopanda kila mwaka.

Alisema kuwa utaratibu huo upo Kisheria na Mkulima asiyetekeleza jukumu hilo hapaswi kulima tumbaku.
Mkoba aliwataka viongozi wa AMCOS kuhakikisha wanawahimiza wanachama wao kutekeleza matakwa hayo ya kisheria kwani kinyume cha hapo ni uvunjaji wa Sheria na viongozi ambao watashindwa kuwasimamia wanachama wa watachukuliwa hatua.
Aliongeza kuwa bila miti hakuna tumbaku , hivyo ni vema wakaitikia wito wa viongozi ili waweze kuendelea kulima zao hilo ambalo ni zao kuu la biashara kwao.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Urambo Adam Malunkwi alimuomba Mkuu wa Mkoa wa Tabora kuwachukulia hatua wakulima wa tumbaku ambao wamekuwa wakivunja Sheria ya kuwataka kupanda miti 250 kabla ya kulima ili iwe fundisho kwa wengine.
Alisema kuwa hatua ikichukuliwa kwa wale wanaopuuzia basi itakuwa fundisho kwa wengi kutii na kuanza kupanda miti.

No comments: