Advertisements

Thursday, March 15, 2018

Lissu awekewa chuma mguuni

Mbunge wa Singida Mashariki (Chadema), Tundu Lissu amewekewa chuma katika mguu wake wa kulia ili kuimarisha mfupa wa paja.
Rais huyo wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS) jana Machi 14, 2018 alifanyiwa upasuaji wa mguu wa kulia kama alivyoshauriwa na madaktari wa Hospitali ya Chuo Kikuu cha Leuven, Gasthuisberg nchini Ubelgiji.
Akizungumza leo na Mwananchi Machi 15, 2018, Lissu amesema operesheni hiyo iliyochukua saa mbili ilifanywa na timu ya madaktari bingwa chini ya uongozi wa Profesa Willem-Jan Mertsemakers.
“Operesheni ilienda vizuri na kwa sasa naendelea na dawa na mapumziko hospitalini kwa muda wa angalau wiki tatu zinazokuja,” amesema Lissu.
“Wameniwekea chuma cha kuimarisha mfupa wote wa paja la kulia. Pia wamechukua vipimo ili kuangalia kama hakuna tatizo la bacteria kabla hawajafunga kabisa sehemu ya kwenye goti ambayo haijaunga hadi sasa.”
Mke wa Lissu, Alicia amesema anamshukuru Mungu kwamba upasuaji huo umekwenda vyema.

No comments: