Advertisements

Monday, May 21, 2018

Sugu Atinga Rasmi Bungeni, Wapinzani Walipuka kwa Furaha

Mbunge wa Mbeya Mjini (Chadema), Joseph Mbilinyi maarufu Sugu, ameingia bungeni kwa mara ya kwanza leo Mei 21, 2018 tangu aachiwe kwa msamaha wa Rais John Magufuli, Mei 10 mwaka huu.

Baada ya kuingia bungeni, wabunge wa upinzani walilipuka kwa furaha wakimshangilia huku wakigonga meza zao kwa takriban dakika mbili, hali iliyosimamisha shughuli za Bunge kwa muda.

Sugu ameingia ukumbini saa 3:20 asubuhi akiwa ameambatana na mbunge wa Viti Maalumu (Chadema), Kunti Yusuph ambaye alisikika akisema: "Leo bungeni ni Sugu tu."

Wakati anaingia, naibu waziri wa Tamisemi, Josephat Kandege alikuwa anajibu maswali ya wabunge, lakini akalazimika kunyamaza kwanza.

Sugu alikwenda moja kwa moja kwa mbunge wa Mtama, Nape Nnauye na kumpa mkono kisha  kwa  waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Ajira, Kazi na Watu wenye Ulemavu,  Jenister Mhagama na kumpa mkono.


Alielekea kwa mwanasheria mkuu wa Serikali, Dk Adelardus Kilangi na waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Utumishi na Utawala Bora), George Mkuchika akawapa mikopo.

Baada ya hapo akarudi upande wake wa upinzani na kukumbatiana na mbunge wa Rombo (Chadema), Joseph Selasini na kwenda kukaa sehemu yake karibu na mbunge wa Tarime Mjini (Chadema), Esther Matiko.

Mwenyekiti wa Bunge, Andrew Change aliwaomba wabunge kutulia ili shughuli za Bunge ziendelee, huku akiwatishia kuwa hatawapa nafasi ya kuuliza maswali ya nyongeza.

“Imetosha sasa, imetosha, haya endelea,” alisema Chenge

No comments: