Advertisements

Thursday, November 15, 2018

GST YAAGIZWA KUANDAA RAMANI ZA MADINI NGAZI ZA MIKOA, WILAYA

 Naibu Waziri wa Madini Doto Biteko, akionesha taarifa ya utafiti wa jiokemia uliofanywa nchi mzima na Taasisi ya Jiolojia ya Madini Tanzania (GST) kwa kushirikiana na Taasisi ya Jiolojia ya China. Kulia ni Mtendaji Mkuu wa Taasisi ya Jiolojia ya China Profesa Sun Xiaoming na Kushoto ni Kaimu Katibu Mkuu Wizara ya Madini, Mathias Absai.
 Naibu Waziri wa Madini Doto Biteko katika picha ya pamoja na ujumbe kutoka Taasisi ya Jilojia ya China, Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini Tanzania (GST), na Wataalam kutoka Wizara ya Madini na Tume ya Madini.
 Naibu Waziri Doto Biteko akimkabidhi Mtendaji Mkuu wa Taasisi ya Jiolojia ya China, Profesa Sun Xiaoming Cheti cha kutambua mchango wake na kukamilika kwa utafiti wa Jiokemia uliofanywa nchini.
 Mtendaji Mkuu wa Taasisi ya Jiolojia ya China, Profesa Sun Xiaoming (kulia) akitoa taarifa ya utafiti huo. Katikati ni Naibu Waziri wa Madini Doto Biteko na kushoto ni Kaimu Katibu Mkuu, Mathias Abisai.

 Sehemu ya Wataalam kutoka Taasisi ya Jiolojia ya China, Wizara, Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini Tanzania (GST) na Tume ya Madini wakifuatilia kikao hicho.
 Mkurugenzi Mtendaji wa GST, Yokobeth Myumbilwa akizungumza jambo katika kikao hicho. 
 Naibu Waziri wa Madini Doto Biteko akizungumza jambo (katikati). Kulia ni Mtendaji Mkuu wa Taasisi ya Jiolojia ya China, Profesa Sun Xiaoming na kushoto ni Kaimu Katibu Mkuu Mathias Abisai.
Naibu Waziri wa Madini Doto Biteko akionesha Taarifa ya Utafiti wa Jiokemia iliyofanywa katika Mkoa wa Mbeya. Kulia ni Mtendaji Mkuu wa Taasisi ya Jiolojia ya China, Profesa Sun Xiaoming na kushoto ni Kaimu Katibu Mkuu Mathias Abisai.

*Biteko asema wachimbaji sasa kuchimba kwa uhakika

Na Asteria Muhozya, Dodoma
Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini Tanzania  (GST) imetakiwa kuandaa ramani zinazoonyesha madini mbalimbali katika ngazi ya Mikoa na Wilaya ili kuwapa nafuu watanzania wanaofanya shughuli za uchimbaji wa madini nchini.
Kauli hiyo imetolewa na Naibu Waziri wa Madini Doto Biteko   baada ya kupokea taarifa ya Utafiti wa Jiokemia katika skeli kubwa na skeli ndogo (Geochemical Mapping for High and Low Density) uliofanyika nchi nzima kwa ushirikiano kati ya GST na Taasisi ya Jiolojia ya China.
Naibu Waziri Doto pia, ameitaka taasisi hiyo kuelekeza nguvu katika kuisaidia serikali katika kupata matokeo chanya katika shughuli za madini huku ikiongeza thamani ya kazi kutokana na utafiti huo na kuongeza kuwa, GST inaweza kutumia utafiti huo mkubwa kuandaa ramani za madini katika ngazi za Mikoa na Wilaya.
 Akizungumzia manufaa ya tafiti huo kwa Tanzania, amesema baada ya muda si mrefu watanzania wanaofanya shughuli za uchimbaji watahamia katika uchimbaji wa uhakika na siyo wa kubahatisha kwa kuwa utafiti huo unaonesha mahali sahihi ambapo shughuli hizo zinaweza kufanywa.
Amesema mbali na shughuli za madini, utafiti huo pia unaweza kutumika katika sekta za kilimo, maji na ujenzi wa barabara kwa kuwa unawezesha kutambua aina ya udongo unaofaa kwa shughuli hizo. 
Kutokana na umuhimu wa utafiti na kazi iliyofanywa na taasisi hizo mbili, Naibu Waziri Biteko ametoa wito kwa Watanzania kuitumia taasisi ya GST katika shughuli za kitaalam ikiwemo kupata taarifa za utafiti zinazohusu sekta ya madini na kuongeza kuwa, sekta hiyo inao uwezo mkubwa wa kutekeleza wajibu wake.
Aidha, Naibu Waziri Doto ametumia fursa hiyo kuishukuru Serikali ya China kutokana na ushirikiano huo iliyoutoa katika kutekeleza utafiti  huo ambao umegarimu kiasi cha Dola za Kimarekani Milioni 4 na Laki Tano 
Kwa upande wake, Mtendaji Mkuu wa Taasisi ya Jilojia ya China, Profesa Sun Xiaoming amesema kuwa taarifa ya utafiti iliyowasilishwa ni ya nchi nzima ya Tanzania na eneo la Mkoa wa Mbeya.
Amesema utafiti huo umetoa matokeo ya jiokemia ya sampuli 71 nchini kote na sampuli 39 katika mkoa wa Mbeya na kuongeza kuwa utafiti huo utasaidia katika utekelezaji maendeleo ya shughuli za madini, kilimo na mazingira nchini.
Awali, akizungumza katika kikao hicho, Kaimu Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini, Mathias Abisai amesema kusudio la ujumbe huo ilikuwa ni kuhakiki kazi iliyofanyika na kuwasilisha ripoti. Ameongeza kuwa, ripoti hiyo itasaidia kwenye tafiti nyingine za madini ikiwemo maji na mazingira.
Ameongeza kuwa, mnamo Mwaka 2009 serikali ya China na Tanzania kwa kutumia taasisi zake za Jiolojia zilisaini hati ya makubaliano (MoU) kwa lengo la kuanzisha mradi huo wa miaka mitano ambapo kazi rasmi ya mradi ilianza mwaka 2013 na kukamilishwa mwaka 2018.

Naye, Kaimu Mtendaji Mkuu wa GST, Yokobeth Myumbilwa akileza malengo ya utafiti huo amesema kuwa ni kupata taarifa za utafiti wa jiokemia kwa ajili ya kuandaa kanzidata ambayo itaainisha uwepo wa taarifa zinazo ainisha uwepo wa aina mbalimbali za madini ,upangaji miji ,pamoja na taarifa hizo kuweza kutumika katika shughuli mbalimbali katika  sekta za kilimo  na mazingira.

No comments: