Advertisements

Wednesday, August 21, 2019

Mbaroni kwa Tuhuma za Kumuua Mkewe

JESHI la Polisi Mkoa wa Arusha linamshikilia dereva wa kampuni ya utalii ya Mt Kilimanjaro Safari’s, Julius Kabora (45), kwa tuhuma za mauaji ya mke wake Rehema Elihudi (31)mkazi wa Kijiji cha Saitabahu wilayani Arumeru mkoani hapa.

Akithibitisha jana ofisini kwake kutokea kwa tukio hilo, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha, Jonathan Shana, alisema Rehema alikutwa chumbani kwake akiwa sakafuni Agosti 19, majira ya saa 4 usiku chumbani kwake akiwa amefariki.

Kwa mujibu wa kamanda Shana katika chumba hicho walikuta mtandio uliokuwa umetundikwa juu ya paa la chumba hicho, huku mwili huo ukiwa na jeraha mdomoni.

Alisema taarifa za kifo cha marehemu zilitolewa polisi na mume huyo wanayeishi nyumba moja na marehemu, lakini kila mtu analala chumba chake na kwamba baada ya kufika nyumbani hapo majira ya saa 4:00 usiku alichungulia ndani ya chumba cha mkewe na kumkuta akiwa amelala chini na baada ya kumwangalia alibaini kwamba amefariki.

“Tunamshikilia mume wa marehmu kwa ajili ya mahojiano zaidi wakati uchunguzi wa kina ukiendelea ili tuweze kubaini kama kweli marehemu amejiua au ameuawa kwa sababu katika nyumba hiyo alikuwa anaishi na mume wake na hawaishi na mtu mwingine,” alisema.

Kamanda Shana aliwakaribisha wananchi wote wenye taarifa zinahusiana na kifo hicho ofisini ili kubaini ukweli wa tukio hilo na kwamba majina yao yatahifadhiwa.

“Ni mapema mno kueleza kilichosababisha chanzo cha kifo hiki, lakini makachero wetu wanaendelea na uchunguzi, milango ya ofisi yangu ipo wazi niwakaribishe wananchi wote wenye taarifa ya mauaji haya kuzileta kwangu,” alisisitiza.

Kwa mujibu wa majirani walioshuhudia mwili huo ukiwa sakafuni baada ya mume huyo kupiga kelele za kuomba msaada ambao hawakutaka majina yao yaandikwe gazetini, walidai walimkuta marehemu akiwa amelala chini huku pembeni yake kukiwa na Biblia, mtandio na simu yake ya kiganjani

GPL

No comments: