Advertisements

Tuesday, October 15, 2019

WAZIRI LUKUVI AWATAKA WAKAZI WA JIMBO LA ISMANI KUSHIRIKI UCHAGUZI WA SERIKALI ZA MITAA

Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi William Lukuvi ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Isimani akiwa anajiandikisha kwenye daftari la mpiga kura katika kituo cha Msindi kilichopo katika kijiji cha Idodi kata ya Idodi kwa ajili ya uchaguzi wa serikali za mitaa 
 Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi William Lukuvi ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Isimani akiwa yupo kwenye mstari kwa ajili ya kujiandikisha kwenye daftari la mpiga kura

NA FREDY MGUNDA,IRINGA.

Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi William Lukuvi ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Isimani  amewataka wakazi wa jimbo hilo kujitokeza kwa wingi kujiandikisha kwenye daftari la mpiga kura kwa siku tatu ambazo zimebakia kwa ajili ya uchaguzi wa serikali za mitaa utakao fanyika tarehe 24-11-2019 na kuhakikisha wanajitokeza kugombea nafasi mbalimbali za uongozi wakati ukifika.

Akizungumza wakati alipokuwa anajiandikisha kwenye daftari za mpiga kura katika kituo cha Msindi kilichopo katika kijiji cha Idodi kata ya Idodi, lukuvi alisema kuwa kila mkazi wa jimbo la Ismani wanahaki wa kujitokeza kujiandikisha na kupata haki ya kumchagua kiongozi wanaemtaka.

“Hii ni fursa pekee ya kuhakikisha unapata nafasi ya kumchagua kiongozi ambaye atasaidia kukuletea maendeleo kwenye mtaa au kijiji chako kwa kipindi cha miaka mitano hivyo wakazi wote nawaomba mjitokeze kwa wingi kujiandikisha” alisema lukuvi

Aidha lukuvi aliwakumbusha vijana kuhakikisha wanajitokeza kwa wingi kujiandikisha,kupiga kura na kugombea nafasi mbalimbali za kiuongozi kwa kuwa nao wanahaki ya kuwa viongozi wa kuongoza mitaa ambayo wanaishi kwa maendeleo ya jamii.

Lukuvi aliupongeza uongozi wa mkoa wa Iringa kwa kuhamasisisha vilivyo zoezi hili la kujiandikisha kwenye daftari la mpiga kura na kufanikiwa kuongoza kitaifa.

Nao baadhi ya wakazi wa jimbo la Ismani waliojitokeza kujiandikisha kwenye Daftari la mpiga kura walimpongeza mbunge huyo kwa kujitokeza na kupanga kwenye mstari kwa ajili ya kujiandikisha kwenye daftari hilo la mpiga kura.

No comments: