Advertisements

Friday, November 22, 2019

Madhara ya Wapenzi Kugombana na Kununiana Mara kwa Mara

MWISHONI mwa wiki iliyopita, nilipata bahati ya kukutana na mmoja kati ya wasomaji wangu wa siku nyingi ambaye amekuwa akiufuatilia ukurasa huu na kujifunza mambo mbalimbali.

Alikuwa na shida iliyomfanya anitafute na alichonieleza, ni kwamba alikuwa akiujutia moyo wake kwa sababu alikuwa amemfanyia kosa kubwa mume wake kwa sababu ya hasira na sasa nafsi yake ilikuwa ikimsuta.

Kibaya zaidi, dhambi aliyokuwa ameifanya, ilikuwa imemnogea kiasi cha kuhatarisha ndoa yake. “Mimi na mume wangu tumekuwa tukigombana mara kwa mara na kibaya zaidi ni kwamba tunapogombana, inachukua muda mrefu sana kumaliza tofauti zetu. Wakati mwingine tunakaa hata mwezi mzima tukiwa tumenuniana ndani ya nyumba, yaani hata salamu hakuna.

“Miezi michache iliyopita, mimi na mume wangu tuligombana na hiyo ilikuwa ni baada ya mimi kukuta meseji kwenye simu yake, ambayo inaonesha inatoka kwa mwanamke ambaye wana mazoea ya kupitiliza. Nilipomhoji, alinijia juu na ugomvi mkubwa ukazuka kati yetu na tukanuniana kwa muda wa wiki mbili.

Katika kipindi ambacho tumenuniana, nilikutana na kaka mmoja ambaye tulikuwa tukifahamiana, lakini tukapotezana kwa muda mrefu. Tangu zamani alikuwa akinitongoza, lakini kwa kuwa mimi ni mke wa mtu, nilikuwa ninamkatalia,” hayo ni maelezo ya msomaji wangu ambaye ameomba nilihifadhi jina lake.

Akaendelea kunieleza kwamba kwa sababu alikuwa na upweke na mawazo mengi kwa kipindi hicho, alijikuta akiangukia kwenye mikono ya mwanaume huyo ambaye alimuonesha mapenzi ya hali ya juu, akawa anataka kujua ni nini kilichokuwa kinamsumbua mpaka muda wote aonekane kuwa ni mwenye

Kuifanya stori iwe fupi ni kwamba mwisho wa yote, dada huyu alijikuta akiangukia dhambini na mwanaume huyu, wakakutana kimwili. Baada ya hapo, mwanaume alizidisha mapenzi maradufu, akawa anampigia simu mara kwa mara, wakawa wanaonana mara kwa mara kiasi cha kujikuta na yeye ameanza kumpenda.

Mumewe alipokuja kuanza kutaka suluhu, tayari mwenzake alikuwa amekolea kwenye penzi la kijana huyu! Wakayamaliza, lakini huo haukuwa mwisho wa dada yetu huyu kutoka kimapenzi na huyu kijana.

Ikawa wakigombana na mumewe tu, basi anaendelea na mchepuko wake na wameendelea hivyo kwa miezi kadhaa kiasi kwamba imefika mahali, mwanamke anamuona mwanaume wa nje ni bora kuliko mumewe wa ndoa kwa sababu kwanza hawajawahi kugombana na anampa mapenzi motomoto kila wanapokutana.

Ungepewa nafasi ya kumshauri dada yetu huyu, ungempa ushauri gani? Mpaka hapo umeona madhara ya kugombana mara kwa mara na kununiana ndani ya nyumba? Tukutane wiki ijayo ambapo tutaendelea na mada hii, nitumie ushauri wako kwa meseji za kawaida au WhatsApp kwa namba hizo hapo juu na wiki ijayo nitakueleza namna ya kuepuka usipate matatizo kama yaliyompata dada huyu.

Usikose wiki ijayo.GPL

No comments: