Advertisements

Wednesday, December 4, 2019

BREAKING: SUMAYE ATANGAZA KUJITOA CHADEMA LEO, AANIKA KASORO ZAO.

WAZIRI mkuu mstaafu, Frederick Sumaye. leo Desemba 4, 2019 ametangaza rasmi kujitoa katika Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema).

“Kuanzia leo nimejiondoa rasmi, mimi sio mwanachama tena wa Chadema, sitajiunga na chama kingine cha siasa. Sijawahi kuwa kibaraka wa chama chochote cha siasa, mnisamehe, nimewasamehe,” amesema katika mkutano na waandishi wa habari.

“Najua katika kujikosha yatakuwepo maneno kama kapewa fedha na CCM au ACT … kama nilipokuja Chadema nilipewa pesa basi na safari hii nimepewa fedha ingawa sijui na nani maana sijiungi na chama chochote.

“Kujiunga upinzani sio jambo rahisi hasa kwa mtu ambaye ulikuwa kwenye nafasi ya juu (uwaziri mkuu) baada ya kujiunga huko nilipata misukosuko, mashamba yangu yaliuzwa na hata familia yangu ilinilaumu sana lakini nilipambana na baadaye familia ikazoea


“Mbowe aliwahi kutupa nasaha kuwa tusiionje sumu kwa kuilamba, na mimi siwezi kuigusa sumu kwa kuilamba, leo natangaza rasmi kuwa sitoendelea kugombea kwenye nafasi ya uenyekiti taifa Chadema.

“Nilipochukua tu fomu ya kugombea uenyekiti wa Chadema taifa, nongwa zikaanza, mimi nilichukua fomu ili kuonesha kuwa demokrasia ipo Chadema tofauti na maneno yanayosemwa mitaani kuwa ukigusa kiti kile tu ni shida.

“Nafasi ya Mwenyekiti, Freeman Mbowe haiguswi, mimi nilitaka kuonyesha kuwa hilo sio kweli lakini nilikuwa najidanganya, nimefanyiwa figisu kwenye uchaguzi wa kanda kisa niligusa kiti cha uenyekiti taifa.

“Baadhi ya wajumbe wa Kamati Kuu ya Chadema ambao walifanya mpango wa mimi kuletewa fomu, ya kugombea mwenyekiti wa kanda ya upinzani, haohao ndiyo walishirikishwa katika kuniangusha. Niliwaambia wajumbe kuwa mkifanya kama mlivyotaka kufanya, nitauthitibitishia umma kuwa ndani ya Chadema hakuna demokrasia ya kweli, au kiti cha Mbowe kina utaratibu mwingine

“Walionifanyia figisu kwenye uchaguzi wa Kanda ya Pwani wamethibitisha kuwa chama hiki ni mali ya Freeman Mbowe na namtahadharisha Mbowe kuwa hilo genge ambalo linamzunguka akidhani linamsaidia ndio linakiumiza chama.

“Sikutoka CCM mwaka 2015 kwa kugombana na mtu wala CCM. Nilihamia upinzani ili kuipa nguvu CCM , na nilisema kuhama kwangu CCM kutawapa nguvu CCM kwani hawatalala usingizi kwa sababu upinzani watakuwa wanawakabili,” amesema Sumaye.

No comments: