Katibu Mkuu wa Chama cha Mapinduzi CCM Taifa Daniel Chongolo amewataka Wakuu wa shule zote zilizochini ya Jumuiya za Chama hicho kuhakikisha wanazingatia miongozo ya uendeshaji wa shule na kusimamia ubora wa kiwango cha elimu ili ziwe shindani na shule nyingine.
Hayo ameyasema Julai 15,2022 wakati akifungua Mkutano wa Wakuu wa Shule za Sekondari zilizochini ya Jumuiya ya Wazazi wa CCM waliokutana Jijini Dodoma kwa lengo la kufanya tathmini ya utendaji kazi katika shule hizo.
Chongolo amesema shule hizo zinatakiwa kuwa mfano katika uendeshaji wake, ufaulu na katika maadili.
“Sasa hivi hatupo tena kwenye giza,tunatakiwa kuongeza bidii kwenye haya mafanikio tuliyoyaleta wenyewe na lazima mfahamu kuwa hakuna muujiza kwenye mafanikio,”amesema
Amesema ili kuendana na malengo ya kuanzisha shule hizo inatakiwa kila kundi lipewe dozi kulingana na hali halisi ya madaraja yao na kwamba kila jambo linahitaji msukumu zaidi wa mafanikio .
“Ahadi yangu ipo palepele kuhakikisha walimu wanakuwa na mazingira mazuri zaidi ili kuendana na hadhi ya Jumuiya hii ikiwa ni pamoja na kuongeza madarasa mawili mawili,tutaangalia pia uhitaji wa shule husika hali itakayoongeza ufanisi na kupekelea shule zetu kuwa kimbilio kwa kila mtu,”amefafanua Chongolo
Aidha Chongolo amewataka Wakuu hao kupenda kufanya kazi kwenye mazingira yanayohitaji mafanikio na kukemea tabia ya baadhi ya walimu kutamani shule zilizofanikiwa.
Katika Hatua nyingine Chongolo amesema serikali imeongeza fursa za upatikanaji wa mikopo ikiwamo kupunguza masharti ya kupata mikopo na wataweka mkazo katika kuzalisha wataalamu wa lugha ya Kiswahili na ukalimani.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wazazi CCM Taifa Dkt. Edimund Mndolwa amesema kwa sasa kumekuwa na mabadiliko makubwa katika shule zilizochini ya jumuiya hiyo hasa katika ufaulu, huku mwenyekiti wa kamati ndogo ya mitihani katika shule hizo mwalimu Jacob Msigwa akaelezea mafanikio waliyoyapata.
”Kwa sasa shule zetu zina utulivu wa kutosha tofauti na ilivyokuwa mwanzo na kueleza kuwa hali hiyo imetokana na maelekezo ya uongozi uliopo na kufanya matokeo mazuri
kwa shule zote za wazazi licha ya wanafunzi waliopo ni wale wanaodhaniwa kuwa hawafundishiki’amesema Dk.Mndolwa

No comments:
Post a Comment