Njombe
Madiwani wa halmashauri ya mji wa Njombe wamepiga marufuku wadau na washirika mbalimbali kwenda kuomba mafuta katika halmashauri hiyo bila utaratibu maalum kwa madai kuwa halmashauri imepata madhara makubwa hususani katika mapato na matumizi ya halmashauri.
Edwirn Mwanzinga na Urick Msemwa ni baadhi ya madiwani wa halmashauri walioibua hoja wakieleza kuwa kila wadau wanapohitaji mafuta wamekuwa wakifika katika halmashauri yao na kudai kuwa kuna wakati vimekutwa vibali vya mafuta kwenye magari ya watu binafsi kinyume na utaratibu,huku pia wakiomba madereva kuzima magari baada ya viongozi kushuka ili kupunguza matumizi makubwa ya mafuta.
“Halmashauri imegeuka kuwa hazina kila mmoja anayetaka mafuta anakuja,hatuwezi kwenda kwa mfumo huo.Tulishaweka utaratibu kwa washirika wetu kuwa yeyote anayetaka mafuta aende kwa mkuu wa wilaya kwa kuwa yeye ndiye anayejua ana halmashauri zake tatu”alisema Edwirn Mwanzinga
Afisa utumishi wa halmashauri Bi. Ester Gama amekiri baadhi ya magari binafsi yakiwemo ya watumishi kujazwa mafuta kwa madai kuwa hatua hiyo imetokana na baadhi ya magari ya serikali kwa wakati huo kushindwa kufanya kazi huku mkurugenzi wa halmashauri Bi.Kuruthum Sadick akibainisha kuwa tayari hatua za udhibiti wa mafuta zimeanza kuchukuliwa na kuwaomba wadau kufuata utaratibu wa kuomba msaada wa mafuta ikiwemo kupitia ofisi ya mkuu wa wilaya.

No comments:
Post a Comment