Advertisements

Wednesday, April 10, 2024

DKT. JAFO: SERIKALI KUTOA TATHMINI YA AMAZINGIRA HIVI KARIBUNI


Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Dkt. Selemani Jafo amesema Serikali inatarajia kutoa taarifa ya tathmini ya mazingira hivi karibuni kubaini maeneo yanayokabiliwa na changamoto za mazingira.

Amesema hayo wakati akijibu swali la Mbunge wa Mwera Mhe. Zahor Mohammed Haji aliyetaka kujua kuhusu Serikali kuelimisha wananchi kujiepusha na madhara yatokanayo na athari za mabadiliko ya tabianchi hadi pale maafa yanapotokea.

Akiendelea kujibu swali hilo, Dkt. Jafo amesema kuwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imekuwa ikichukua hatua mbalimbali kwa kuelimisha wananchi kuhusu madhara yanayotokana na mabadiliko ya tabianchi ili waweze kujilinda na maafa.

Waziri Dkt. Jafo ametaja baadhi ya hatua hizo kuwa ni pamoja na kutoa elimu kupitia njia mbalimbali hasa vyombo vya habari na mitandao ya kijamii.

“Mheshimiwa Naibu Spika, elimu inayotolewa inalenga kukuza uelewa kwa makundi mbalimbali katika jamii hasa wakulima, wavuvi, na wafugaji kuhusu mbinu bora za kilimo, ufugaji na uvuvi endelevu zinazoweza kupunguza athari za mabadiliko ya tabianchi lakini pia kujilinda na maafa yanayoweza kutokea kwa jamii” amesema.

Katika hatua nyingine Mhe. Dkt. Jafo ametoa wito kwa Mamlaka za Serikali za Mitaa kuangalia namna ya kuvisaidia vikundi vya uzalishaji wa miche ili viwezeze kuzalisha kwa wingi.

Ametoa wito huo wakati akijibu swali la nyongeza la Mbunge wa Lulindi Mhe. Issa Mchungahela aliyetaka kujua hatua ya serikali ya kujengea uwezo vikundi vinahamasisha mazingira.

No comments: