Wednesday, June 26, 2024

TOENI TAARIFA WANAOFANYA UKATILI KWA WENYE CHANGAMOTO YA NGOZI, TUTAENDELEA KUWALINDA MVUNGWE.


Mkaguzi Kata ya Mvungwe Wilaya ya Kilindi Mkoa wa Tanga amebainisha kuwa wataendelea kuwalinda wenye changamoto za ulemavu wa Ngozi huku akiwaomba wananchi kutoa taarifa za baadhi ya watu ambao wanafanya ukatili huo.

Hayo yamebainishwa na Mkaguzi wa kata hiyo Mkaguzi Msaidizi wa Polisi A/INSP Fabian Mhagale ambapo amewataka wananchi wa kata hiyo kushirikiana na Jeshi la Polisi Kwa kutoa Taarifa za uhalifu na wahalifu huku akiwaomba wananchi wenye changamoto za ulemavu wa Ngozi kutambua kuwa kata hiyo inashirikiana na Mkaguzi huyo pamoja na vikundi vya ulinzi shirikishi ili kuhakikisha wako salama wao na mali zao.

Mkaguzi huyo amebainisha kuwa kutokana na tukio la hivi karibuni huko Mkoani Kagera la kuuawa Kwa Mtoto mwenye changamoto ya Ngozi amewaomba wananchi wa kata hiyo kutokuwa na hofu kwani kata hiyo imeendelea kuboresha ulinzi kwa watu wenye changamoto hiyo pamoja na vikundi vya ulinzi shirikishi na vile vya kukusanya taarifa za watu wenye nia ya kufanya ukatili huo.

A/Insp Mhagale amesisitiza kuwa aliona ni vyema kuwafikia Familia ya Bwana Idd ambaye familia yake ina changamoto hiyo ambapo amewaambia kuwa yeye na familia yake wako salama ambapo amemuomba kutumia vyema mawasiliano yake pindi watakapo kuwa na mashaka na watu wasio waamini katani hapo Juu ya usalama wao.

Mkaguzi huyo pia amebainisha kuwa wanaanchi wanapaswa kushiriki kikamilifu katika ulinzi wa watu wenye changamoto ya Ngozi ambapo ameweka wazi kuwa kata yake haitomuonea muhali mtu yoyote atakayebainika kufanya ukatili huo.

Vilevile amewaomba wananchi wa kata ya Mvungwe Wilaya ya Kilindi Mkoa wa Tanga kuendelea kushirikiana na viongozi wa kata hiyo ili kuwabaini wahalifu na uhalifu ndani ya kata hiyo.

No comments: