Advertisements

Saturday, June 29, 2024

WAZIRI SIMBACHAWENE AMPONGEZA RAIS KWA KUTEKELEZA MIRADI YA MAENDELEO INAYOWAGUSA WANANCHI WOTE


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. George Simbachawene na Mbunge wa Jimbo la Kibakwe amempongeza Rais Mhe. Samia Suluhu Hassan katika kipindi chake cha uongozi kwa kujipambanua kutoa fedha nyingi kwa ajili ya kutekeleza miradi ya maendeleo inayowagusa wananchi wa chini moja kwa moja

Ametoa kauli hiyo leo wakati Mwenge wa Uhuru ukiwa katika Kijiji cha Itende Kata ya Pwaga wilayani Mpwapwa Mkoani Dodoma ambapo umekagua na kuweka jiwe la msingi katika Mradi wa Maji wenye thamani ya Shilingi Bilioni 4 utakaohudumia vijiji vitatu pamoja na vitongoji vitatu
Akizungumzia utekelezaji wa Mradi huo wa maji, Mhe. Simbachawene amesema shabaha ya Rais Mhe. Samia Suluhu Hassan ni kuona huduma za msingi ikiwemo maji yanapatikana kwa urahisi bila kulazimika wananchi kusafiri umbali mrefu kuifuata huduma hiyo

Katika hatua nyingine Mwenge wa Uhuru ukiwa katika Kata ya Rudi wilayani humo umekagua utekelezaji wa shughuli mbalimbali ikiwemo uwekaji wa jiwe la msingi kwenye jengo la maabara lililotekelezwa kwa thamani ya Sh. Milioni 94.
Awali, akizungumza Kiongozi wa Mbio za Mwenge Kitaifa, Bw. Godfrey Mzava ameridhishwa na utekelezaji wa mradi wa maji huku akisema taratibu zote za manunuzi zilifuatwa wakati wa utekelezaji wa mradi huo.

Bw.Mnzava amesema Mhe.Rais amedhamiria kuhakikisha huduma za kijamii ikiwemo maji umeme ziapatikana kwa wananchi wote bila kujali mahali walipo

Ameongeza kuwa Agenda kuu ya Mbio za Mwenge mwaka huu ni kutunza mazingira na kuhamasisha ushiriki wa uchaguzi wa mitaa
Kwa mujibu wa taarifa Mwenge wa Uhuru Mkoani Dodoma unapita kukagua idadi ya miradi 56 yenye thamani ya Sh.Bilioni 21.2 ambapo utakimbizwa kwa siku nane katika wilaya saba Mkoa huo kwa umbali wa kilomita 1484

Mwenge wa Uhuru kwa mwaka huu unaongoza na kauli mbiu ya ‘’Tunza Mazingira na Shiriki Uchaguzi wa Serikali za Mitaa kwa Ujenzi wa Taifa endelevu’’

No comments: