Wednesday, July 3, 2024

MBETO : AWATA WANASIASA KUFUATA NYAYO ZA MHE.NASSOR MAZRUI


Na.Mwandishi Wetu - ZANZIBAR.
KATIBU wa Kamati Maalum ya NEC,Idara ya Itikadi,Uenezi na Mafunzo CCM Zanzibar Khamis Mbeto Khamis, amewataka wanasiasa nchini kuwa wangwana na kufuata nyayo za Waziri wa Afya Zanzibar Nassor Ahmed Mazrui aliyekiri na kusifu kazi kubwa inayofanywa na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Hussein Mwinyi kwa kusimamia kwa ufanisi utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi CCM ya mwaka 2020/2025 katika sekta ya Afya nchini.

Kauli hiyo ameitoa katika mahojiano maalum huko Afisini kwake Kisiwandui Zanzibar, alisema kasi ya utendaji wa Rais wa Zanzibar Dk.Hussein Mwinyi katika kuimarisha sekta mbali mbali nchini hasa Wizara ya Afya imevuka malengo ya Ilani ya CCM.

Mbeto, alisema kitendo cha "Waziri wa Afya ambaye pia ni Naibu Katibu Mkuu wa Chama Cha ACT-Wazalendo Nassor Ahmed Mazrui jana katika ufunguzi na makabidhiano ya nyumba za wafanyakazi hospitali ya Abdulla Mzee Mkoa wa Kusini Pemba kukiri na kupongeza kasi ya utendaji wa Dk.Mwinyi ni uzalendo mkubwa unaotakiwa kuwa fundisho kwa wanasiasa wengine nchini kujitathimini kisiasa,kimaono na kifikra.

Alisema kitendo cha kiongozi huyo mkuu wa Chama cha upinzani nchini kujitokeza hadharani kusifu utekelezaji wa Ilani ya CCM ya mwaka 2020/2025 katika Wizara ya Afya ni salamu za pekee kwa vyama vya upinzani nchini kuwa CCM itashinda kwa kishindo katika uchaguzi mkuu ujao.

Katika maelezo yake Mbeto, alifafanua kuwa Waziri huyo Mazrui alimsihi Dkt.Mwinyi aendelee kufanya kazi wala asijali maneno ya watu kwani utendaji wake unaonekana kwa wananchi.

"Chama Cha Mapinduzi Zanzibar tunaposema hatuna mbadala wa Dk.Mwinyi tunaimanisha kwani kazi tuliyopewa na wananchi ya kuleta maendeleo endelevu tayari imefanyika katika sekta mbalimbali tunachosubiri ni wananchi kujaza visanduku vya kura nyingi za ndio kwa nafasi za Rais,Wabunge,Wawakilishi na Madiwani wa CCM.

Kuona kiongozi wa timu ya mkakati ya Chama cha ACT-Wazalendo Nassor Mazrui anamsifu Rais Dk.Mwinyi sio jambo dogo kuna kazi kubwa imefanyika mpaka kuweka mbele uzalendo badala ya kubeza na kukosoa.", alisema Mbeto.
Mbeto,alisema katika sekta ya afya Serikali imejenga "ujenzi wa hospitali za kisasa za Wilaya 10 kila wilaya pia hospitali kubwa ya Mkoa yenye vifaa tiba vya kisasa nchini.

Alifafanua kuwa serikali ya awamu ya nane ya Zanzibar chini ya uongozi wa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Hussein Mwinyi, imetekeleza mambo mengi ya maendeleo ikiwemo kufikisha huduma ya umeme kwa gharama nafuu,ujenzi wa barabara za kisasa,ujenzi wa skuli,kuongeza pencheni kwa wazee,kuongeza mishahara kwa watumishi wa umma pamoja na kuimarisha miundombinu ya sekta binafsi.

No comments: