Sunday, July 15, 2012

TUNDU LISU MATATANI TENA BUNGENI

MNADHIMU wa Kambi ya Upinzani Bungeni, Tundu Lissu ameingia matatani kutokana na kauli yake kwamba Rais Jakaya Kikwete amekuwa akiteua majaji wa Mahakama Kuu wasiopendekezwa na Tume ya Utumishi wa Mahakama.

Kutokana na kauli hiyo aliyoitoa wakati akiwasilisha maoni ya kambi yake, kuhusu hotuba ya makadirio ya matumizi ya Wizara ya Katiba na Sheria, Lissu ambaye pia ni Mbunge wa Singida Mashariki (Chadema) atajadiliwa na Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge.

Wakati akisoma hotuba yake, mbunge hiyo alisema majaji wanaoteuliwa na Rais hawafanyiwi ‘vetting’ (uchunguzi) na tume hiyo kuona kama uwezo na ujuzi wao unafaa kukabidhiwa madaraka ya ujaji.
Mwenyekiti wa Bunge, Jenista Mhagama ndiye aliyeamuru suala la Lissu kupelekwa katika kamati hiyo baada ya mbunge huyo kukataa kufuta kauli yake ambayo kwa mtazamo wa Serikali iliwadhalilisha majaji.

Hata hivyo, jana alipotakiwa kueleza kama ana taarifa rasmi za kuitwa kwenye kamati hiyo Lissu alisema: “Sijaitwa, lakini nina taarifa kuwa naweza kuitwa.’’

Alisema, hata wakimwita hatakuwa na jambo lolote la kuzungumza kwa kuwa Mwenyekiti wa Bunge aliyeongoza kikao hicho juzi (Jenista Mhagama), alikosea kwa kuwa ndiye aliyepaswa kumpa adhabu.
Mbunge huyo alisema  juzi aligoma kufuta kauli yake kama alivyotakiwa na Mwenyekiti kwani aliamini kuwa hata Mwanasheria Mkuu alikuwa amekosea.
Alibainisha kuwa endapo ataitwa katika kamati hiyo, atahoji kama waliomwita wamegeuka kuwa wenyeviti wa Bunge na kama si hivyo, anaamini watakosa neno la kumhoji.
Waziri wa Katiba na Sheria, Mathias Chikawe na Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Jaji Frederick Werema kwa nyakati tofauti wakati wakijibu hoja za wabunge juzi jioni walisema: “Lissu aliwakashifu majaji bungeni, hivyo alipaswa kuomba radhi.”

No comments: