Tuesday, March 26, 2013

Polisi yawaonya wanaosambaza uvumi wa Pasaka

Dar es Salaam. Polisi imeonya kuwachukulia hatua za kisheria wote watakaojihusisha na vurugu kipindi cha Sikukuu za Pasaka, zitakazoadhimishwa mwishoni mwa wiki.
Msemaji wa Polisi, Advera Senso alisema wamekamilika na hafikirii kama kutakuwa na yeyote atakayevunja amani.
Senso alikuwa akizungunmzia kuhusu uwapo wa uvumi wa baadhi ya watu kutaka kuvuruga shughuli za ibada kuanzia Alhamisi hadi Jumatatu. “Taarifa hizo kwa kweli hatuna, wanaovumisha uchonganishi huo tunawaonya waache mara moja kwa sababu wanahatarisha amani, tukiwapata tutawachukulia hatua za kisheria,” alisema Senso.
Alisema Tanzania haina udini wala ukabila, ipo salama na ikiwa kuna mwenye ushahidi au taarifa kuhusu kusudio la uhalifu zipeleke polisi, kwani hiyo ndiyo polisi shirikishi. Kuhusu madai ya baadhi ya viongozi wa Kikristo kupeleka taarifa hizo polisi, Senso alisisitiza kuwa Tanzania haina udini na atakayevunja amani kwa namna yoyote atashughulikiwa kisheria kama mhalifu siyo kidini.
Alisema kila mwananchi anatakiwa kujilinda, kulinda mwenzake na taifa lake kwa jumla.
Katibu Mkuu wa Umoja wa Makanisa ya Kipentekoste Tanzania (FPCT), Askofu David Mwasota alilieleza Mwananchi jana kuwa, licha ya taarifa za maandishi zinazosambazwa katika simu za viganjani, wiki iliyopita Wasomali wengi walionekana wakiingia nchini na kwamba taarifu zimefikishwa polisi.

Imeandikwa na Editha Majura, Nuzulack Dausen na Pamela Chilongola
Naye Katibu wa Baraza la Maskofu Tanzania (TEC), Padri Anthony Makunde alikiri kuwapo taarifa za vitisho dhidi ya Wakristo katika maadhimisho ya Pasaka na kwamba, walipeleka taarifa kwenye vyombo vya usalama ili zifanyiwa kazi.
Alitoa wito kwa waumini wote wa dini hiyo watakaopokea ujumbe wa vitisho vya aina hiyo, wapeleke taarifa kwenye vituo vya polisi kwa sababu ndiyo wenye jukumu la kushughulikia usalama wao.
“Ni jukumu la polisi kuhakikisha usalama wa raia na mali zao, tunaiamini Serikali yetu na kwa kuwa tumeishawapelekea taarifa, waumini wasiogope wahudhurie ibada za maadhimisho ya Pasaka kama kawaida,” alieleza Padri Makunde.
Mkurugenzi wa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), Dk Hellen Kijo-Bisimba alitoa wito kwa vyombo vya dola kuimarisha ulinzi na kuchukua hatua dhidi ya wanaosambaza taarifa kwa njia mbalimbali, zenye lengo la kusababisha hofu kwa watu.
“Watanzania wawe macho, wasipuuze hata kidogo taarifa zinazosambazwa kwa kuwa hakuna anayejua kama vitisho hivyo vinaweza kutekelezwa au la, hivyo kila mwananchi anatakiwa kuwa makini na kujilinda,” alisema Dk Bisimba.
Ibada za Pasaka
Kwa mujibu wa taarifa zilizotolewa na Mtendaji wa Mawasiliano Jamii wa TEC, Padri Salawa Anatoly ibada ya Pasaka ya Jumapili kitaifa itafanyika Dodoma katika Kanisa Kuu la Mtakatifu Paulo wa Msalaba, ikiongozwa na Askofu wa Jimbo hilo, Gervas Nyaisonga.
Naye Ofisa wa Programu ya Habari na Mawasiliano wa Jumuiya ya Kikristo Tanzania (CCT), Mchungaji John Kamoyo alisema ibada ya Ijumaa Kuu kitaifa

itafanyika Kanisa la Kiinjili la Kilutheli (KKKT) Dodoma.
Kwa upande wa FPCT, Askofu Mwasota alisema kutakuwa na ibada ya kilele cha kuliombea taifa, kwenye ukumbi wa ukumbi wa PTA, Sabasaba; kuanzia asubuhi mpaka jioni.
Mwananchi

No comments: