Advertisements

Tuesday, April 21, 2015

UTAMU NA CHUNGU YA PENZI NI 50%

Kama ilivyo ada wapenzi wasomaji wa safu hii karibuni kwa Jumanne nyingine katika kuelimishana na kujuzana kuhusu uhusianao na maisha.Kabla sijaanza mada ya wiki hii napenda kuwakumbusha mada ya wiki iliyopita kutamani au kuwa na mtu anayekufaa wakati wewe mwenye hujajitathmini kama unamfaa

Ni matumaini yangu wasomaji wangu mtakuwa mmejifunza mengi kuhusu mada iliyopita, leo nitazungumza nanyi kuhusu utamu na uchungu wa penzi kwa watu wote.Ukibahatika kusikiliza maongezi ya watu wa jinsia ya kike dhidi ya jinsia ya kiume utasikia maneno haya; Hawa wanaume mama yao ni mmoja, tabia na matendo yao ni yaleyale hawana maana yoyote hata umbebe vipi sawa na kazi bure atakusaliti tu. Hata kama utakuwa unamuosha na kumbeba mgongoni, ng’o! bado haridhiki sijui wameumbwaje? Lazima atachepuka tu.

Hali kadhalika ukisikiliza mazungumzo ya upande wa walalamikiwa (wanaume) utagundua nao wanawalalamikia wanawake kuwa ndiyo wanaongoza kwa kuwaumiza, kuwasaliti, kuwagombanisha na mengineyo.Mfano;Utasikia akisema wanawake tunaishi nao tu, ila ni viumbe dhaifu, tena dhaifu sana wenye kulaghaika muda wowote, hawana mapenzi ya dhati hata kama utampa kila kitu, tena nafuu wanawake wale wa zamani kuliko hawa wa sasa, hawa ni pasua kichwa.

Ukijaribu kulinganisha wanachokizungumzia pande zote mbili, kila mtu anavutia upande wake dhidi ya mwenzie, lakini ukweli huko hivi; Wapo wanaume wenye mapenzi ya dhati na kweli wasio wasaliti kwa wapenzi wao lakini wapenzi wao wanaweza kuwa wachepukaji wazuri sana.

Hata kwa wanawake wapo walioumbwa na mapenzi ya dhati na ya kweli wasio wasaliti lakini wenza wao ni viwembe ile mbaya.Kuna wanaume na wanawake wanaofurahia uhusiano wao wa kimapenzi kwa kupendana kuheshimiana na kuelewana ndani ya nyumba, huku wengine wakiumizana kila kukicha kutokana na kusalitiana.

Ukichukua asilimia ya wanawake na wanaume wanaofurahia uhusiano wao kisha ukachukua asilimia ya wanaume na wanawake wanaoteseka katika uhusiano uleule, utagundua utamu na chungu ya penzi ni asilimia 50 kwa kila upande.

Ni mara chache sana wapenzi wenye tabia linganifu kuoana, mara nyingi kama mwanamke au mwanaume ni mpole basi mwenza wake atakuwa mkorofi, mlevi, mgomvi au si muaminifu.
Tukutane wiki ijayo katika mada nyingine nzuri zaidi.

GPL

No comments: