Advertisements

Wednesday, June 21, 2017

Hakimu kortini kwa rushwa

HAKIMU wa Mahakama ya Mwanzo Magomeni, Omary Abdallah na mfanyabiashara George Balongo wamefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam wakikabiliwa na mashitaka manne yakiwemo ya kushawishi rushwa ya Sh milioni moja na kupokea rushwa ya Sh 500,000.

Washitakiwa hao walifikishwa mahakamani hapo jana na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), mbele ya Hakimu Mkazi, Respicious Mwijage. Mwendesha Mashitaka wa Takukuru, Emmanuel Jacob alidai jana kuwa washitakiwa hao wanakabiliwa na mashitaka manne waliyoomba kutoka kwa Agness Nyanze ili wamsaidie katika kesi ya mirathi.

Jacob alidai katika mashitaka ya kwanza yanayomkabili Abdallah, inadaiwa katri ya Januari na Februari 12, mwaka huu, katika maeneo yasiyofahamika jijini Dar es Salaam, akiwa mtumishi wa mahakama kama hakimu, aliomba rushwa ya Sh 205,000 kutoka kwa Nyanze ili amsaidie katika kesi ya mirathi namba 570/2016.

Katika mashitaka ya pili, inadaiwa Februari 12, mwaka huu maeneo yasiyofahamika jijini humo, Abdallah alipokearushwa ya Sh 205,000 kutoka kwa Nyanze. Pia inadaiwa kati ya Februari na Machi mwaka huu, washitakiwa wote walishawishi na kuomba rushwa ya Sh milioni moja kutoka kwa Nyanze ili wamsaidie katika kesi hiyo ya mirathi. Jacob alidai Machi Mosi mwaka huu, hakimu huyo (Abdallah) na mfanyabiashara walipokea rushwa ya Sh 500,000 kutoka kwa Nyanze ili wamsaidie katika shauri la mirathi.

Washitakiwa walikana mashitaka na upande wa mashitaka ulidai kuwa upelelezi wa kesi hiyo haujakamilika na kwamba hawana pingamizi na dhamana endapo washitakiwa watakithi masharti ya dhamana. Hata hivyo, Hakimu Mwijage aliwataka washitakiwa kila mmoja kuwa na mdhamini mmoja mwenye barua ya utambulisho kutoka taasisi za serikali au ofisi yoyote iliyosajiliwa kisheria atakayesaini kulipa Sh milioni 10.

Mshitakiwa Abdallah alitimiza masharti hayo na kuachiwa huru hata hivyo, mshitakiwa Balongo alirudishwa rumande kwa kushindwa kutimiza masharti hayo. Kesi itatajwa Julai 4, mwaka huu.

HABARI LEO

No comments: