Advertisements

Saturday, March 24, 2018

Baba Ahukumia Jela Miaka Minne kwa Kosa la Kumpa Mimba Binti yake

Mahakama ya Hakimu Mkazi wa Mkoa wa Tabora imemhukumu mkazi wa Manispaa ya Tabora, Sadick Masunzu (47) kifungo cha miaka minne jela baada ya kupatikana na hatia ya kumbaka binti yake mwenye umri wa miaka 16 na kumpatia ujauzito.

Akitoa hukumu hiyo jana, hakimu wa mahakama hiyo, Joctan Rushela alisema ameridhika na maelezo yaliyotolewa na upande wa mashtaka uliokuwa ukiongozwa na wakili Tito Mwakalinga kuthibitisha bila shaka kuwa mshtakiwa alitenda kosa hilo.

Hakimu huyo aliongeza kuwa kitendo kilichofanywa na mshtakiwa si cha kiungwana katika jamii ya Watanzania, hivyo mahakama inamtia hatiani kwa kosa hilo na inamhukumu kwenda jela miaka minne ili liwe funzo kwake na kwa wengine wenye tabia kama hiyo.

Awali wakili wa Serikali, Mwakalinga alidai mahakamani hapo kuwa mshtakiwa alimbaka mtoto wake wa kumzaa na kumsababishia ujauzito.


Mwakalinga alidai mshtakiwa alitenda kosa hilo katika tarehe tofauti Januari 2017 na kumsababishia ujauzito binti huyo aliyekuwa mwanafunzi wa Sekondari ya Lwanzali iliyopo katika Manispaa ya Tabora ashindwe kuendelea na masomo.

Upande wa mashtaka uliiomba mahakama hiyo kutoa adhabu kali kwa mshtakiwa kwa kuwa kitendo cha kumbaka na kumtia mimba mtoto huyo ambaye ni mwanafunzi kimemharibia maisha yake.

No comments: