Advertisements

Tuesday, July 24, 2018

Sababu tatu za watu 65 kujiua Geita kwa miaka miwili

By Rehema Matowo, Mwananchi rmatowo@mwananchi.co.tz

Geita. Watu kukata tamaa ya maisha, wivu wa mapenzi na ulevi ni miongoni mwa sababu za watu 65 kujiua katika kipindi cha miaka miwili mkoani Geita.

Kwa mujibu wa Shirika la Afya Duniani (WHO), kila mwaka zaidi ya watu 800,000 hujiua duniani.

Katika ripoti yake, WHO inasema kwamba kitendo cha watu kujiua hutokea katika rika zote bila kujali umri na kwa mwaka 2015 pekee, kujiua kulishika nafasi ya pili kwa vifo vyote duniani hasa vya vijana wa umri wa kati ya miaka 15-29.

Katika taarifa yake kwa vyombo vya habari jana, kamanda wa Polisi Mkoa wa Geita, Mponjoli Mwabulambo alisema watu 65 walijiua mkoani humo kuanzia mwaka 2017 hadi Julai 2018.

Alisema mwaka 2017 watu 43 walijiua, wengi wakiwa ni kwa kujinyonga. Alisema tangu Januari hadi Julai mwaka huu, watu 22 wamejiua.

Mwabulambo alisema hayo alipokuwa akizungumzia tukio la hivi karibuni la mfanyabiashara wa madini kujiua kwa kujipiga risasi akiwa kwenye nyumba ya kulala wageni ya Flamingo eneo la Buseresere wilayani Chato.

Kamanda huyo alisema takwimu zinaonyesha wilaya za Chato na Geita zinaongoza kwa matukio hayo katika kipindi hicho yakiwa 24. Matukio ya watu kujiua wilayani Chato mwaka jana yalikuwa 18 na mwaka huu yamefikia sita, wakati Geita ikiwa na matukio 10 mwaka huu tofauti na 14 ya 2017.

Mwabulambo alisema Mbogwe ina matukio tisa huku matano yakiwa ya mwaka jana na manne mwaka huu, ikifuatiwa na Bukombe ambako watu watano wamejiua kati ya hao wanne mwaka 2017 na mmoja mwaka huu. Wilaya ya Nyang’wale ina matukio matatu, mawili yakiwa ya 2017 na moja mwaka huu.

Kamanda alisema matukio ya watu kujiua kwa wivu wa mapenzi takwimu zinaonyesha mwaka jana yalikuwa matano na Januari hadi Julai yako sita.

Alisema matukio ya watu kujiua kwa kukata tamaa ya maisha mwaka 2017 yalikuwa saba na sasa yako matatu.

Kamanda Mwabulambo alisema watu wanne walijiua kutokana na magonjwa ya akili, matukio mawili mwaka jana na mawili mwaka huu.

Alisema matukio yanayohusisha ulevi yalitokea mawili 2017 na kuanzia Januari hadi Machi hakuna lililotokea.

Kuhusu matukio ya watu kujiua kwa sababu nyingine, alisema yalikuwa 38, kati ya hayo 27 yalitokea mwaka jana na mwaka huu yako 11.

Kamanda Mwabulambo alisema mtu anapofikia uamuzi wa kujiua ni wa kuonewa huruma huku akiiomba jamii kuwasaidia kabla ya kufikia hatua ya kujitoa uhai. Alisema watu wa aina hiyo wanahitaji ushauri wa kisaikolojia.

Pia, aliitaka jamii kuwa karibu na ndugu zao wanapowaona wana msongo wa mawazo.

No comments: