Advertisements

Friday, January 10, 2020

Ajali ya ndege ya Ukraine: ‘Iran ilidungua ndege ya Ukraine kimakosa’

Iran
Ushahidi unaashiria kuwa kombora la Iran lilidungua ndege ya abiria ya Ukrain iliyoanguka karibu na Tehran, kimakosa, viongozi wa magharibi wanasema.

Viongozi wa Canada na Uingereza wanataka uchunguzi wa kina ufanyike kubaini chanzo halisi kilichosababisha, ajali iliyowaua watu wote 176 waliokuwa ndani ya ndege hiyo.

Ukraine awali ilisema kuwa inachunguza endapo ndege yake iliangushwa na kombora, jambo ambalo mamlaka za Iran zilikanusha vikali.

Kuanguka kwa ndege hiyo kulitokea saa chache baada ya Iran kushambulia kambi za kijeshi za Marekani nchini Iraq kwa makombora ya masafa marefu.

Vyombo vya habari vya Marekani vinaashiria ndege hiyo ilidhani kuwa ndege ya kivita ya Marekani wakati Iran ilipokuwa ikijiandaa kujibu mashambulio dhidi ya Marekani baada ya wao kushambulia vituo vyake vya kijeshi nchini Iraq kwa makombora.

Kituo cha habari cha CBS imevinukuu vyanzo vya kijasusi vya Marekani vinavyodai kuwa picha za satelaiti zinaonesha mwanga wa makombora mawili ambao ulifuatiwa na mwanga wa mlipuko.


Kituo cha habari cha CBS imevinukuu vyanzo vya kijasusi vya Marekani vinavyodai kuwa picha za satelaiti zinaonesha mwanga wa makombora mawili ambao ulifuatiwa na mwanga wa mlipuko.

Kanda ya video iliyopatikana na New York Times ilionenesha jinsi makombora yalivyokuwa yakipita katika anga la Tehran na baadae kulipuka ilipokutana na ndege.

Karibu sekunde 10 baadae mlipuko mkubwa ulisikika ardhini. Ndege iliyoshika moto, inaendelea kupaa.

Rais wa Marekani Donald Trump siku ya Alhamisi alisema: "nina mashaka" juu ya (kuanguka) kwa ndege. "Inawezekana kuna mtu amefanya kosa kubwa."

Iran imetangaza kutokabidhi kisanduku cheusi cha kuhifadhi taarifa za ndege kwa kampuni ya ndege ya Boeing ama serikali ya Marekani kwa uchunguzi wa ajali hiyo.

Hatua hiyo inatokana na mzozo uliokomaa baina ya Marekani na Iran, hasa baada ya Trump kuagiza shambulio la anga lililomuua Jenerali wa Iran Qasem Soleimani Januari 3.

Chini ya sheria za kimataifa za usafiri wa anga, Iran ina haki ya kuongoza uchunguzi wa ajali hiyo lakini kawaida huwa kampuni iliyotengeneza ndege pia hushirikishwa kwa karibu.

Ndege hiyo ni Boeing 737-800 ambayo imetengenezwa Marekani, nchi ambayo ni hasimu wa Marekani.

CBS na Newsweek waliripoti kuwa maafisa wa ujasusi wa Marekani na Iraq wana hakika kuwa ndege hiyo iliangushwa na makombora ya Iran.

CBS wamechapisha taarifa inayodai kuwa mitambo ya rada ya Marekani ilibaini makombora mawili yakirushwa muda mfupi kabla ya ndege hiyo kulipuka.Kwa upande wa Newsweek wamewanukuu maafisa wa Marekani na Iraq ambao wanaamini ndege hiyo ilidunguliwa na makombora ya Kirusi aina ya Tor M-1 ambayo Nato huyaita Gauntlet.

Maafisa wawili kutoka makao makuu ya jeshi la Marekani wameithibitishia Newsweek kuwa shambulio hilo lilikuwa la bahati mbaya.

ran imesema nini?

Mkuu wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga wa Iran Ali Abedzadeh amesema: " Ndege hiyo ambayo awali ilikuwa ikielekea magharibi baada ya kupaa ilikata kona kulia kutokana na hitilafu ya kiufundi na ilikuwa ikirejea uwanja wa ndege pindi ilipoanguka."

Abedzadeh ameongeza kuwa mashuhuda waliona ndege hiyo "ikiwaka moto" kabla ya kuanguka na kuwa marubani hawakutoa taarifa yoyote ya dharura kabla ya kujaribu kurudi uwanja wa ndege wa Imam Khomeini.

"Ndege kadhaa za ndani na nje zilikuwa zikipaa katika anga la Iran katika usawa wa futi 8,000 (kama ndege ya Ukraine). Hivyo suala la kupigwa na makombora haliwezi kuwa na ukweli wowote," ameongeza.

Afisa huyo amedai kuwa taarifa za awali za uchunguzi zimeshapelekwa Ukraine na Marekani, ambapo ndipo makao makuu ya Boeing.

Taarifa hizo pia zimepelekwa Sweden na Canada ambao pia wamepoteza raia wao.

No comments: