Advertisements

Friday, May 20, 2022

MACHINGA KUTUNGIWA SHERIA YA KUWALINDA


Katibu Mkuu Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Dkt. Zainab Chaula akizungumza wakati akifunga mafunzo ya siku nne ya wafanyabiashara ndogo ndogo maarufu Machinga, katika Ukumbi wa Jakaya Kikwete Dodoma Mei 19, 2022.
Baadhi ya washiriki wa Mafunzo ya wafanyabiashara ndogo ndogo, maarufu Machinga wakifuatilia siku ya mwisho ya mafunzo hayo katika Ukumbi wa Jakaya Kikwete Dodoma Mei 19, 2022.
Katibu Mkuu Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Dkt. Zainab Chaula akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya Viongozi wa Shirikisho la Umoja wa Machinga kutoka Mikoa na Halmashauri mara baada ya mafunzo ya wafanyabiashara ndogo ndogo maarufu Machinga, katika siku ya mwisho ya mafunzo hayo, Ukumbi wa Jakaya Kikwete Dodoma Mei 19, 2022.Picha zote na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini WMJJWM

Na WMJJWM Dodoma
Katibu Mkuu Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Dkt. Zainab Chaula amesema Serikali imeanza mchakato wa kutunga Sheria ya kuwalinda wafanyabiashara ndogo ndogo maarufu kama 'machinga'.

Dkt. Zainab ametoa kauli hiyo jijini Dodoma Mei 19, 2022 wakati akifunga mafunzo kwa viongozi wa Shirikisho la Umoja wa Machinga Tanzania (SHIUMA).

Katika hatua nyingine Dkt. Chaula ametumia nafasi hiyo kutoa mwezi mmoja kwa mikoa ambayo haijakamilisha usajili wa wanachama wa Shirikisho hilo kufanya hivyo ili kuwepo takwimu sahihi za wanachama zitakazosaidia kuhudumia kundi hilo.

Dkt. Chaula ameongeza kuwa shabaha ya Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Mhe. Samia Suluhu Hassan ni kuhakikisha kundi la machinga linaratibiwa vizuri na linapata fursa mbalimbali za kiuchumi ikiwemo mikopo na masoko ya bidhaa zao.

"Ndio maana Rais Samia akaunda Wizara hii na kuipa jukumu la kuratibu makundi Maalum ikiwepo kundi la Machinga kwa sababu Serikali inawajali na kuwathamini Machinga kama yalivyo Makundi mengine waliopo ndani ya jamii' alisema Dkt. Chaula

Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum kwa kushirikiana na wadau wengine wakiwemo Shirika la Posta, NSSF, ASAS na wadau wengine waliandaa mafunzo kwa viongozi wa Shirikisho la Umoja wa Machinga nchini kwa lengo la kuwajengea uwezo katika masuala ya uongozi na kuweka mikakati ya uendeshwaji Shirikisho lao.

No comments: