Advertisements

Thursday, July 6, 2023

BODI YA WAKURUGENZI WA TAWA YAZINDUA MRADI MKUBWA WA MAJI NKONKO MANYONI

Na Beatus Maganja – SINGIDA

Bodi ya Wakurugenzi wa Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA) imezindua mradi mkubwa wa maji unaogharimu shillingi Millioni 400 katika Kijiji cha Nkonko kilichopo kata ya Nkonko Wilaya ya Manyoni Mkoani Singida

Mradi huo unaoelezwa kuzalisha Lita 2,000 za maji Kwa saa na kutarajiwa kuwanufaisha wananchi zaidi ya 8,000 na taasisi mbalimbali za Serikali ikiwemo shule ya Sekondari yenye jumla ya wanafunzi 200 na walimu 14 umezinduliwa leo Julai 5, 2023 na Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa TAWA Mej. Jen. (Mstaafu) Hamis Semfuko

Akizungumza katika hafla ya Uzinduzi wa mradi huo, Mwenyekiti huyo amesema TAWA imeamua kuunga mkono juhudi za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan katika kutatua tatizo la miundombinu ya maji linalowakabili wananchi.

“Sisi TAWA tumeamua kuunga mkono juhudi za Mhe. Rais katika kutatua tatizo hili kubwa la maji hapa nchini, tumefanya hivyo Kwa vitendo kama mnavyoona hapa na maeneo mengine lakini vilevile tumefanya hivyo Kwa kununua gari letu wenyewe la kuchimba maji” amesema

Mej. Jen. (Mstaafu) Semfuko amesisitiza kuwa TAWA chini ya Serikali ya Rais Samia imedhamiria kupunguza changamoto Kwa wananchi katika maeneo yote yaliyo katika usimamizi wao

“Moja ya tatizo la Taifa letu ni miundombinu ya maji na ndio maana TAWA katika maeneo yote tutakayokaa tutahakikisha kwamba tunatoa huduma hiyo Kwa wananchi ” amesisitiza

Akitoa shukrani zake Kwa niaba ya wananchi, diwani wa kata ya Nkonko Mhe. Ezekiel Ezekiel amesema wananchi wanajivunia uwepo wa TAWA katika eneo lao kwani kupitia taasisi hiyo wamepata manufaa makubwa ikiwemo mradi mkubwa wa maji, kukamilishwa Kwa ujenzi wa hosteli ya wasichana katika shule ya Sekondari kutokana na asilimia 20 ya fedha wanazopata kupitia shughuli za Uwindaji wa Kitalii unaofanywa maeneo hayo na msaada wa haraka wanapovamiwa na wanyama Wakali na Waharibifu

Sambamba na Uzinduzi wa mradi huo, bodi ya Wakurugenzi wa TAWA ilitembelea na kukagua mradi wa barabara yenye urefu wa Kilometa 142 inayotengenezwa ndani ya Pori la Akiba Kizigo Kwa mashirikiano kati ya TAWA na Wadau wa Uhifadhi WCS na EBN pamoja na kupokea jumla ya viti 10 vya walemavu vyenye thamani ya shillingi 8,000,000/= (Millioni Nane) kutoka Kwa mwekezaji Nicolas Negre wa EBN Hunting Safari Ltd

Naye Kamishna wa Uhifadhi wa TAWA Mabula Misungwi Nyanda, amewapongeza Wadau wa Uhifadhi WCS na EBN Kwa ushirikiano mkubwa wanaoutoa Kwa Taasisi anayoisimamia (TAWA) unaofanikisha shughuli za ulinzi na Uhifadhi katika Pori la Akiba kizigo na kuwasihi waendeleze mashirikiano hayo Kwa mustakabali wa Pori hilo na Uhifadhi Kwa ujumla Nchini.

Pia amempongeza Kamanda wa Pori hilo, Oggosy Gasaya Kwa kazi nzuri anayoifanya na Kwa ushirikiano mzuri anaoutoa Kwa wananchi wanaozunguka Pori hilo pamoja na Wadau wa uhifadhi

No comments: