Wednesday, April 3, 2024

MARUFUKU KUINGIZA MAGARI MABOVU BARABARANI


Na Issa Mwadangala
Madereva mkoani Songwe wametakiwa kuacha tabia ya kuendesha magari mabovu kimazoea ambayo yanaweza kuhatarisha maisha yao na kuleta madhara kwa watumiaji wengine wa barabara.

Hayo yamesemwa na Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP) Nassoro Sisiwayah, Mkuu wa operesheni kikosi cha usalama barabarani nchini April 01, 2024 alipofanya ukaguzi katika kituo cha ukaguzi wa vyombo vya moto kilichopo Chimbuya mkoani Songwe
ACP Sisiwayah alisema “dereva unatakiwa kujali usalama wako kwanza kisha kuwajali watumiaji wengine wa barabara ili kuweza kujiepusha na madhara ambayo yanaweza kuepukika, ingiza gari barabarani likiwa zima na sio kuingiza gari bovu ambalo linakufanya usiwe na uhakika na safari uendayo mtambue kuwa sheria haijalala tunawachukulia hatua kwa makosa yote mliofanya ili iwe fundisho kwa wengine wenye tabia kama hii” alisema Kamanda Sisiwayah.

Kwa upande wake Mkuu wa Kikosi cha usalama barabarani Mkoa wa Songwe Mrakibu Mwandamizi wa Polisi SSP Charles Bukombe amewataka madereva kutii sheria bila shuruti na sio kushtukizwa na operesheni kama hizi.

"fuateni sheria za usalama barabarani, ni ajabu kuona dereva aliyepitia mafunzo ya usafirishaji kushindwa kutii sheria kwa makusudi na kusababisha ajali, fuateni sheria ili kulinda miundombinu, jamii, watumiaji wa barabara na nyinyi wenyewe kwa manufaa ya taifa letu" alisisitiza Mrakibu Mwandamizi wa Polisi Bukombe.

No comments: