Sunday, July 21, 2024

WAZIRI WA KILIMO ATEMBELEA SKIMU YA UMWAGILIAJI YA USENSE KATAVI


Mhe. Hussein Bashe (Mb), Waziri wa Kilimo ameendelea na ziara yake ya kikazi na kukagua mradi wa ukarabati wa skimu ya umwagiliaji ya Usense, mkoani Katavi tarehe 20 Julai 2024 na kuongea na wanakijiji wanufaika wa mradi huo.
Mradi wa Usense upo katika eneo la ukubwa wa hekta 106 ambapo Waziri Bashe amewaambia wanakijiji malengo ya Serikali ni kuboresha na kuongeza huduma mbalimbali kwa ustawi wa jamii zao.

Amewaeleza malengo hayo ni kuanza ujenzi wa awamu mbili wa kuvuta mkondo wa maji kupitia ujenzi wa mfereji wa maji; na baadae bwawa la maji ili kurahisisha shughuli za umwagiliaji wa kilimo.
Katika kufanikisha awamu hizo mbili, Waziri Bashe amemwelekeza Bw. Raymond Mndolwa, Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Taifa ya Umwagiliaji (NIRC) kutengeneza daraja la kivuko ambalo litawezesha wakulima kuwa na umbali wa kilomita 1.8 kufanya shughuli za kilimo cha umwagiliaji badala ya kutembea umbali wa kilomita 7 ambazo wamekuwa wakitembea hadi sasa.

Waziri Bashe ameomba wanakijiji hao wasiuze ardhi ili miradi hiyo iwe na manufaa makubwa kwa familia zao na vizazi vijavyo. Aidha, Waziri Bashe anaendelea na ziara yake mkoani Kigoma tarehe 21 Julai 2024 ambapo atakagua mradi wa umwagiliaji wa Lueche mkoani humo.



No comments: