Friday, October 18, 2024

OFISI YA MAKAMU WA RAIS KUSIMAMIA MAZINGIRA MIKOANI

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji akifafanua hoja za wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Maji na Mazingira wakati akiwasilisha taarifa ya Udhibiti wa Utiririshaji wa Majitaka na Taka za Viwandani katika Ziwa Victoria jijini Dodoma leo Oktoba 17, 2024.

Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Maji na Mazingira Mhe. Jackson Kiswaga akizungumza wakati wa kikao cha kupokea na kujadili taarifa ya Udhibiti wa Utiririshaji wa Majitaka na Taka za Viwandani katika Ziwa Victoria jijini Dodoma leo Oktoba 17, 2024.
Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Khamis Hamza Khamis akifafanua hoja za wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Maji na Mazingira wakati akiwasilisha taarifa ya Udhibiti wa Utiririshaji wa Majitaka na Taka za Viwandani katika Ziwa Victoria jijini Dodoma leo Oktoba 17, 2024.
Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais Mhandisi Cyprian Luhemeja akizungumza wakati wa kikao cha kupokea na kujadili taarifa ya Udhibiti wa Utiririshaji wa Majitaka na Taka za Viwandani katika Ziwa Victoria jijini Dodoma leo Oktoba 17, 2024.
Naibu Katibu Mkuu (Mazingira) Ofisi ya Makamu wa Rais Bi. Christina Mndeme akizungumza wakati wa kikao cha kupokea na kujadili taarifa ya Udhibiti wa Utiririshaji wa Majitaka na Taka za Viwandani katika Ziwa Victoria jijini Dodoma leo Oktoba 17, 2024.

Ofisi ya Makamu wa Rais inatarajia kuanzisha mfumo wa kuwa na afisa atakayefanya kazi ya kufuatilia shughuli mbalimbali za mazingira zinazofanyika katika eneo husika.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji ameiarifu Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Maji na Mazingira wakati akiwasilisha taarifa ya Udhibiti wa Utiririshaji wa Majitaka na Taka za Viwandani katika Ziwa Victoria jijini Dodoma leo Oktoba 17, 2024.

Amesema maafisa walioteuliwa kwa kazi hiyo, pamoja na mambo mbalimbali watashirikiana na watalaam wa kanda za Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazngira (NEMC) ambao ni wasimamizi wa sheria pamoja wataalamu wa ngazi za mikoa kufuatilia na kuzitafutia ufumbuzi changamoto zilizopo katika maeneo hayo.

Akijibu hoja za wajumbe kuhusu uchafuzi wa mazingira unaotokana na taka ngumu, amesema Mhe. Dkt. Kijaji amebainisha kuwa Serikali itazifanyia kazi changamoto hizo kwa kuendelea kutoa elimu hususan kuhusu agenda ya kutenganisha taka.

“Tumepanga kuanzisha mifumo ya kielektroniki ya ukusanyaji wa taarifa za mazingira nchini ili kuwa na kanzidata katika masuala ya taka ngumu na taka hatarishi, hivyo tutakuwa tunatengeneza muelekeo chanya kwa taifa letu katika masuala ya hifadhi ya mazingira,” amesisitiza.

Mhe. Dkt. Kijaji ameongeza kuwa Ofisi ya Makamu wa Rais itaendelea kukuza dhana ya uchumi mzunguko ili kuchochea matumizi ya taka zinazozalishwa kuwa malighafi hatua itakayodhibiti taka ngumu kuzagaa na kuchochea usafi wa mazingira.

Katika hatua nyingine, amesema Ofisi inakamilisha taratibu za kuanzisha Kituo cha Mfano mkoani Geita kitakachoratibu mafunzo kuhusu matumizi sahihi ya teknolojia mbadala za matumizi ya zebaki.

Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Maji na Mazingira Mhe. Jackson Kiswaga ameshauri kuwa na mtaalamu wa mazingira katika migodi na viwanda liwe ni takwa la kisheria ili usimamizi uwe endelevu.

Amesema kuwa pia kuna umuhimu wa kushirikiana kwa ukaribu na halmashauri zote nchini ili usimamizi wa mazingira uweze kuyafikia maeneo mbalimbali.

Mhe. Kiswaga ambaye pia ni mbunge wa Kalenga amesisitiza kulinda mazingira ya Ziwa Victoria ambalo lina umuhimu mkubwa kwa Maisha ya wananchi.

Kwa upande wake Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais Mhandisi Cyprian Luhemeja amesema kwa vile suala la mazingira ni mtambuka, ameteuliwa mtaalamu atakayesimamia wizara zote za kisekta kuhakikisha usimamizi wa mazingira unakuwa endelevu.

Amesema mtaalamu huyo atashirikiana na NEMC Kanda kusimamia viwanda na migodi kubaini changamoto zozote za kimazingira inazokuwa nazo na kuzipatia ufumbuzi.

“Mtaalamu anayeteuliwa kusimamia wizara hizo atakuwa na wajibu wa kutoa elimu kuhusu kulinda mazingira na kutoa adhabu kwa wanaokiuka sheria ya mazingira,” amesema Mhandisi Luhemeja.

Wakichangia taarifa hiyo, baadhi ya wajumbe wakiwemo Mhe. Prof. Shukurani Manya, Mhe. Agnes Hokororo na Mhe. Soud Mohammed Jumah wameelezea umuhimu wa kuwa na mifumo ya kutenganisha taka ngumu.

Wamesema kuwa suala la kutenganisha taka ngumu lianzie ngazi ya familia hadi hadi ngazi ya taasisi ili kujenga msingi mzuri katika udhibiti wa taka na kuchochea usafi wa mazingira.

No comments: