Advertisements

Wednesday, April 27, 2011

Umewahi kujiuliza, naye anakupenda?

SINA shaka marafiki zangu mtakuwa wazima wa afya njema na sasa mnaendelea na majukumu yenu kama kawaida baada ya kumaliza mapumziko ya siku tano. Tangu Ijumaa hadi jana ilikuwa ni Sikukuu mfululizo!

Ni jambo la kumshukuru Mungu kama sherehe zimemalizika salama bila kukutana na balaa la aina yoyote. Kilichobaki kwa sasa ni kuchapa kazi kwa nguvu ili kusukuma mbele gurudumu la maisha.
Leo nimekuandalia mada nzuri ambayo nina imani baada ya kumaliza kuisoma utakuwa na mabadiliko makubwa katika maisha yako ya kimapenzi.



Rafiki yangu, inawezekana upo katika uhusiano na mpenzi wako kwa muda mrefu, lakini hata siku moja hujawahi kufikiria kuhusu penzi lake kwako, anakupenda?
Kumbuka kwamba, hapa nazungumza zaidi na wale ambao wapo na wapenzi wao wanaowapenda kwa dhati. Wewe ndiye unayehusika moja kwa moja na mada yetu ya leo. Unajua kama ni kweli mwenzi uliyenaye yupo moyoni mwako, lazima ufikirie juu ya penzi lake kwako.

Kimsingi hili ni jambo la muhimu sana kwako kulifahamu, unaweza kuwa na mpenzi halafu ghafla ukashangaa amebadilika, haeleweki, hana mapenzi kama zamani, kila siku anakupiga chenga, ukimwuliza msimamo wake hakuweki wazi. Haya ni baadhi ya matatizo ambayo yanawakumba na kuwaacha njia panda wengi bila kufahamu nia halisi ya mpenzi wako.

Unaweza kuwa na mpenzi wako, lakini mambo yake yakakuweka mahali ukashindwa kupata picha kuwa, anakupenda au ana nia ya kukufanya chombo cha starehe kisha kuachana na wewe.
Katika mapenzi hili ni tatizo kubwa sana linalowasumbua wengi, hususan wanawake.
Hata hivyo, kuna vitu ambavyo ukiwa makini kumchunguza mpenzi wako utaweza kujua kama anakupenda au anakupotezea muda wako.

Wakati mwingine unaweza kumuuliza mpenzi wako kama anakupenda kwa dhati na jibu lake likaendelea kuwa, anakupenda sana. Hayo ni maneno ya kutoka midomoni tu, lazima upate muda wa kuchunguza ili kujua kama kile kinachotoka kinywani mwake kinawakilisha kilicho ndani ya moyo wake.
Hapa nimekuandalia mambo ya msingi kuyachunguza ili kujua kama mpenzi wako ana mapenzi ya dhati, yamepungua au hataki tena kuwa na wewe. Ni rahisi sana, hebu fuatilia uone.

Mawasiliano hulegalega
Hili ni la kwanza kabisa kuonekana kwa mpenzi ambaye hana mapenzi ya dhati au uhusiano umeanza kulegalega. Hana msisimko na simu yako kama zamani, wakati mwingine huona kero hata kupokea.
Chunguza jambo hili kwa makini, kama alikuwa na mazoea ya kukupigia simu mara tatu au zaidi kwa siku, hupunguza taratibu na wakati mwingine huacha kabisa.

Ukimuuliza, jibu atakalokupa halina maana yoyote, wakati mwingine ukimpigia simu huchelewa kupokea au asipokee kabisa! Yote haya husababishwa na mapenzi kupungua au kutoweka kabisa katika moyo wake.

Ukiona mpenzi wako anapunguza mawasiliano na wewe, ujue kuna kitu kinaendelea. Kama alikuwa na kawaida ya kukuandikia sms hupunguza kasi, hata kama akikuandikia inakuwa haina ladha ya mahaba kama ilivyokuwa awali.

Ukimuandikia sms hukujibu kwa mkato, tena jibu tata ambalo litakuacha na maswali mengi yasiyo na majibu. Mfano, umemwandikia sms inayosema: “Nakupeda mpenzi wangu, sina mwingine zaidi yako, lakini naona siku hizi umebadilika sana, kuna nini dear? Hebu niambie msimamo wako barafu wa moyo wangu!” Kwa sms nzuri kama hii, siyo ajabu akajibu: “Kila siku unakuwa na maswali ya jela, kama huamini nakupenda basi...” Huyu hakupendi, anatafuta sababu ya kuachana na wewe.

Anazidisha visingizio
Mpenzi wa aina ninayoizungumzia hapa huwa ana visingizio vingi. Mara nyingi hapendi kukutana na wewe na husingizia kwamba yupo bize na kazi ambazo mwanzoni wakati mkianzisha uhusiano wenu hakuwa nazo!

Mazoea ya kutoka pamoja kama zamani huisha, unapomgusia kuhusu kuwa naye mahali kwa ajili ya kupanga maisha yenu ya baadaye, hukujibu kuwa ana mambo mengi ya kimaisha. Siyo ajabu kukwambia kuwa, yupo makini na mambo ya kimaisha zaidi kuliko kukufikiria wewe.

Hatua hii ni ya mbali zaidi, ukiona mpenzi wako amefikia hapa, ujue kweli hana mapenzi na wewe tena, mtu wa aina hii hata mwanzoni huwa hana mapenzi ila tamaa ya mwili wake humdanganya.
Ukiambiwa kwamba, hana muda wa kufikiria kuhusu wewe, badala yake anawaza mipango mbalimbali ya maisha yake, tafsiri ni kwamba, wewe si sehemu ya maisha yake. Akifikia hapo, utakuwa tayari jibu umeshalipata na wewe utakuwa ndiyo mwamuzi wa mwisho wa nini cha kufanya.

Hataki faragha
Kwa kuwa anajilazimisha kuwa na wewe, hakupendi au ana mpango wa kukuacha, basi hata kukutana na wewe faragha kwake ni mzigo. Ule msisimko aliokuwa nao zamani unatoweka na sasa anakufananisha na rafiki yake wa kawaida.

Ukiona mpenzi wako ambaye alikuwa akipenda sana kukutana na wewe faragha, halafu ghafla amebadilika basi hapo ujue wazi kuwa, huna mtu na kinachokunyemelea ni maumivu ya kuachwa!
Wakati mwingine ukweli huwa unauma sana, lakini ni bora unywe dawa chungu upone. Hapa ndiyo sehemu yako ya kusimama mwenyewe kama mhusika mkuu wa uhusiano wako na kufanya uamuzi sahihi katika maisha.

Joseph Shaluwa ni Mshauri wa Mambo ya Mapenzi ambaye anaandikia magazeti ya Global Publishers, kwa sasa ameandika vitabu vya True Love na Let’s Talk About Love vilivyopo mitaani. Unaweza kumtembelea kwenye mtandao wake; www.shaluwanew.blogspot.com au kujiunga naye kwenye facebook.

No comments: