Advertisements

Tuesday, May 31, 2011

BIZARI: KIUNGO CHA MBOGA CHENYE FAIDA NYINGI-GPL

Inawezekana katika maisha yako hujawahi kula mboga iliyowekwa kiungo kinachoitwa bizari, kama umewahi, inawezekana pia hujawahi kujua faida zake mwilini.

Bizari (Turmeric) ni kiungo cha mboga jamii ya mimea unaochimbwa kama mizizi, mfano wa tangawizi, lakini tangawizi yenyewe ina rangi ya njano na hujulikana pia kama ‘manjano’ kutokana na rangi yake.


Kiungo hiki kinatumiwa sana katika Bara la Asia na hasa India na China. Kutokana na umuhimu wake kiafya, vyakula vingi hupikwa kwa kuchanganya na kiungo hiki ambacho sasa kimeenea dunia nzima, ikiwemo Tanzania.

FAIDA ZA BIZARI KIAFYA
Bizari hutumika na watu wengi kama kiungo cha mboga cha kuongeza ladha katika mchuzi na pengine kuweka rangi, lakini kuna faida nyingi unazozipata unapotumia kiungo hiki kila mara katika mapishi yako.


Inaelezwa kuwa bizari ina virutubisho vyenye uwezo wa kuimarisha kinga ya mwili, mara 8 zaidi ya Vitamin C na Vitamin E, ina uwezo wa kushusha kiwango cha lehemu (cholesterol) na kuzuia mtu kuzeeka kabla ya wakati.
Aidha, bizari huimarisha sehemu za magoti hivyo kukuepusha na matatizo ya miguu kuuma. Bizari pia hun’garisha ngozi na kuifanya kuwa yenye afya na huimarisha pia mfumo wa usagaji chakula (Digestion).


SUALA LA UBORA NI MUHIMU
Katika ulimwengu wa maendeleo ya sayansi na teknolijia tulionao sasa, bizari hutengenezwa viwandani na kuhifadhiwa kwa usafirishaji sehemu mbalimbali duniani na kwa ajili ya matumizi ya muda mrefu. Katika hali kama hiyo, si ajabu kukuta bizari iliyoongezewa kemikali zingine za kuhifahdia chakula.

Bizari ya aina hiyo, tayari inakosa faida zilizoelezwa hapo juu, hivyo ni suala muhimu kuangalia ubora wa bizari unayoitumia na mahali inapotoka. Katika nchi yetu, Mungu ametujaalia ardhi yenye rutuba ambapo kiungo kama hiki kinalimwa na kupatikana kwa wingi na kwa uhalisia wake.

Katika suala la kujali ubora, pendelea zaidi kununua bizari kutoka sokoni ambayo imetengenezwa katika mazingira safi na salama na bila kuchanganywa na kitu kingine. Iwapo pia utanunua bizari iliyokwisha hifadhiwa, ni vyema ukasoma maelezo yake kuona kama haina vikorombwezo (additives) vingine.

 Ni ukweli ulio wazi kuwa ukitumia bizari iliyobora utapa faida nyingi kiafya, hivyo hakikisha katika upikaji wako wa kitoweo cha nyama, kama vile kuku, samaki, ngo’mbe unaweka bizari. Upikaji mzuri ni ule wa kuweka kiungo hicho mwisho baada ya mboga yako kuchemka na kuiva, kwani haitakiwi bizari kuchemka sana.

Kwa ujumla hizi ndizo faida utakazozipata ukiifanya bizari kuwa sehemu ya viungo katika mlo wako wa kila siku:
UTAIMARISHA KINGA YA MWILI WAKO
UTAIMARISHA AFYA YA MACHO
UTAIMARISHA SEHEMU ZA VIUNGIO VYA MWILI WAKO
UTAIMARISHA UTENDAJI KAZI WA INI
UTAIMARISHA CHEMBE HAI ZA MWILI
UTAIMARISHA MFUMO WA USAGAJI CHAKULA
UTAIMARISHA MFUMO WA DAMU MWILINI
UTASHUSHA KIWANGO CHA KOLESTRO MWILINI
UTAIMARISHA MFUMO WA UZALISHAJI MBEGU ZA UZAZI
UTAIMARISHA KIWANGO CHA SUKARI MWILINI.

No comments: